Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 1 Industries and Trade Wizara ya Viwanda , Biashara na Uwekezaji 6 2019-04-02

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-

Wakati wa kampeni Mkoani Morogoro Mheshimiwa Rais aliahidi kumaliza tatizo la ajira kwa vijana kwa kuhakikisha anarudisha viwanda, vilivyokufa na kuwachukulia hatua walioviua ili kurudisha ajira kwa vijana na wanawake:-

Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kuwa viwanda vyote vilivyobinafsishwa visivyofanya kazi vinafufuliwa na kuanza kazi ili vichangie katika uchumi na kutoa ajira kwa vijana. Aidha, Serikali inahamasisha ujenzi wa viwanda vipya kutegemeana na fursa zinazopatikana nchini.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Morogoro una jumla ya viwanda 14 vilivyobinafsishwa, kati ya viwanda hivyo, viwanda nane vinafanya kazi na viwanda sita havifanyi kazi. Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Msajili wa Hazina imefanya tathmini ya viwanda vilivyobinafsishwa nchini
vikiwemo vya Mkoa wa Morogoro na kubaini kuwa baadhi ya wawekezaji hawajatekeleza kikamilifu makubaliano ya mikataba ya mauzo ikiwa ni pamoja na kutofanya uwekezaji kulingana na mpango uliokubaliwa.

Mheshimiwa Spika, kufuatia kutoridhika na baadhi ya wawekezaji ambao hawakutekeleza mikataba ya mauzo kufikia mwezi Februari, 2019, Serikali imetwaa viwanda 14 vilivyobinafsishwa vikiwemo viwanda viwili vya Mkoa wa Morogoro. Viwanda vilivyorejeshwa Serikalini kwa Mkoa wa Morogoro ni Mang’ula Mechanical and Machine Tools na Dakawa Rice Mill Ltd. Kwa sasa viwanda vyote 14 vilivyorejeshwa Serikalini vinaandaliwa utaratibu wa kutafuta wawekezaji wenye uwezo wa kuvifufua. Kiwanda cha Morogoro Canvas Mill Ltd ambacho nacho kimefungwa majadiliano yanaendelea kati ya mwekezaji na Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Msajili wa Hazina, inaendelea kufuatilia kwa karibu viwanda vilivyobaki ambavyo havifanyi kazi vikiwepo viwanda vya Mkoa wa Morogoro ili kuchukua hatua stahiki.