Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 18 2019-04-03

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Primary Question

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE aliuliza:-

Katika kikao cha kazi, Mheshimiwa Rais akiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Hamis Kigwangalla na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega alitoa maelekezo ya kutoondoa Vijiji vilivyomo katika maeneo ya Hifadhi:-

(a) Je, tangazo hilo linamaanisha kuwa wameruhusiwa kuendelea na shughuli za kiuchumi katika maeneo yao wanayoishi?

(b) Je, ni lini sasa Serikali itashughulikia migogoro ya mipaka baina ya Vijiji hivyo na Hifadhi au kwa tamko lile maana yake Wanavijiji waendelee kama vile hakukuwahi kuwa na migogoro?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tarehe 15 Januari, 2019, Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alitoa agizo la kutoviondoa vijiji 366 vilivyoainishwa kuwa na migogoro na maeneo ya hifadhi. Aidha, alisisitiza kwamba agizo hilo halina maana kwamba sasa wananchi wanaruhusiwa kuvamia maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, baada ya Mheshimiwa Rais kutoa maelekezo hayo, Kamati Maalum kwa lengo la kumshauri Mheshimiwa Rais namna bora ya kutekeleza agizo hilo iliundwa. Kamati hii inaongozwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo na Makazi. Wizara nyingine zinazohusika ni Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Wizara ya Maliasili na Utalii, Mifugo, Uvuvi, TAMISEMI, Ulinzi, Kilimo na Maji. Jukumu la Kamati litakapokamilika, taarifa itawasilishwa kwa Mheshimiwa Rais na maelekezo yatatolewa kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kufuatia Kamati kukamilisha kazi yake na taarifa kuwasilishwa kwa Mheshimiwa Rais, Wizara ya Maliasili na Utalii itapitia upya mipaka ya hifadhi mbalimbali kwa kuzingatia ushauri wa Kamati na maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Kazi hii itahusisha uwekaji wa vigingi vipya (beacons) katika mipaka yote.