Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 4 Energy and Minerals Wizara ya Madini 32 2019-04-05

Name

Christopher Kajoro Chizza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buyungu

Primary Question

MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA aliuliza:-

Katika Wilaya ya Kakonko kuna wachimbaji wadogo wa madini aina ya dhahabu katika Vijiji vya Myamwilonge, Nyakayenzi, Ruhuru na kuna dalili za kuwepo madini hayo katika sehemu nyingine. Aidha, kuna madini ya chokaa katika Milima ya Nkongogwa ambayo yana matumizi mengine ya viwandani:-

Je, Serikali imejipangaje kufanya utafiti wa uwepo wa madini na kuwasaidia wachimbaji ili wayachimbe na kujipatia kipato?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda sasa nijibu swali la Mheshimiwa Engineer Christopher Kajoro Chiza, Mbunge wa Buyungu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania ilifanya tafiti zifuatazo:-

(i) Upimaji na utafiti wa jiolojia uliofanyika mwaka 1960 na kuchora ramani ya jiolojia ya QDS (Quarter Degree Sheet) namba 43 pale Kakonko.

(ii) Utafiti wa pili ulifanyika mwaka 1978 – 1980 Serikali ilifanya utafiti wa jiofizikia kwa kutumia ndege na kufanya uchakataji wa takwimu zilizochukuliwa na hatimaye kuainisha maeneo yenye mipasuko ya miamba inayoashiria uwepo wa madini mbalimbali katika maeneo ya Kakonko na taarifa hizo zipo katika Ofisi ya GST (Geological Survey of Tanzania).

(iii) Utafiti wa tatu ulifanywa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ikiwemo Mradi wa Nordic Fund, Kampuni ya Beak Consultants ya Ujerumani na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kati ya mwaka 2003 na 2014 walifanya utafiti wa jiosayansi na kubainisha yafuatayo:-

(a) Uwepo wa madini ya dhahabu katika Kata ya Muhange, Kijiji cha Mwiluzi, Nyamtukuza, Nyamwilonge, Msekwa/ Galama, Kasela na Kata ya Kasuga katika Kijiji cha Nyakayenzi; na;

(b) Madini ya agate katika Kata za Kasanda, Kijiji cha Nkuba, Kata ya Gwanumpu katika Kijiji cha Kabingo na Kata ya Nyamtukuza katika Vijiji vya Nywamwilonge na Kasela.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia Geological Survey of Tanzania inakamilisha uandaaji wa kitabu cha madini yapatikanayo katika toleo la nne ambacho kinaonesha uwepo wa madini katika mikoa, wilaya na vijiji, hivyo kitasaidia wananchi na wachimbaji wadogo katika kutambua madini yaliyopo katika maeneo yao na matumizi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali kupitia Geological Survey of Tanzania itaendelea kufanya tafiti zaidi za kijiosayansi katika mwaka 2019/2020 kwenye maeneo ya Ruhuru na Nkongogwa katika Wilaya ya Kakonko ili kubaini madini yaliyopo katika maeneo hayo. Pia itatoa elimu kwa wachimbaji wadogo kuhusu njia bora za uchimbaji na uchenjuaji ili waweze kuelewa kuhusu jiolojia na madini yaliyopo kwenye maeneo yao na kuwashauri namna bora ya kufanya uchimbaji na uchenjuaji salama wenye tija kwa lengo la kuhakikisha kuwa wananchi wanafaidika na rasilimali ya madini iliyopo katika maeneo yao.