Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 5 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 39 2019-04-08

Name

Rhoda Edward Kunchela

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Katavi

Primary Question

MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-

Serikali iliahidi kumaliza migogoro ya ardhi kwa kupima maeneo ya wananchi mapema ili kuepuka bomoa bomoa bila fidia:-

Je, ni lini jambo hilo litafikia mwisho?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba kila kipande cha ardhi nchini kinatambuliwa, kinapangwa na kinapimwa. Katika kutekeleza azma hiyo, Wizara imenunua vifaa vya kisasa vya upimaji ambavyo vimesambazwa katika kanda zote nane na vinatumiwa na Hamashauri zote ili kurahisisha na kuharakisha upimaji wa maeneo ya wananchi na kutoa hatimiliki za ardhi. Vile vile Wizara inaendelea na utekelezaji wa mkakati wa kupima kila kipande cha ardhi nchini ambapo awamu ya kwanza ya mkakati huu inatekelezwa kupitia Mradi wa Majaribio wa Kuwezesha Umiliki wa Ardhi (Land Tenure Support Programme) unaotekelezwa katika Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi katika Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetoa kiasi cha shilingi 6,400,000,000 kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa 25 kwa ajili ya kupima, kupanga na kumilikisha ardhi. Halmashauri hizo ni Halmashauri ya Jiji la Mbeya, Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Halmashauri ya Sumbawanga, Manispaa ya Shinyanga na Iringa, Halmashauri za Miji ya Makambako, Njombe, Kondoa, Nzega, Kahama, Bariadi na Halmashauri za WIlaya za Misungwi, Sengerema, Geita, Nzega, Bukombe, Magu, Chato, Ukerewe, Busega, Simanjiro, Gairo, Songea, Namtumbo na Itilima. Serikali inaendelea kutafuta fedha katika vyanzo mbalimbali ili jambo hili lifikie mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na utekelezaji wa kupima kila kipande cha ardhi nchini, Wizara imeendelea na utekelezaji wa Programu ya Kurasimisha Makazi yasiyopangwa katika maeneo mbalimbali nchini kwa kushirikiana na makampuni binafsi ya kupanga na kupima ardhi yaliyosajiliwa kwa mujibu wa sheria. Lengo la Serikali ni kuhakikisha maeneo yote yanapangwa na kupimwa ili kukidhi mahitahi ya sasa na ya baadaye na hivyo kuzuia uendelezaji holela ambapo husababisha migogoro na adha kwa wananchi ikiwemo bomoa bomoa ya makazi yasiyo rasmi.