Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 6 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 48 2019-04-09

Name

Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Primary Question

MHE. ANTONY C. KOMU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya mara kwa mara ya kuyapima upya mashamba yaliyotaifishwa wakati wa Azimio la Arusha ambayo hivi sasa yamebadilishwa matumizi na kujengwa Shule, Zahanati, Hospitali, Makazi na kadhalika?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Antony Calist Komu, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna mashamba kadhaa nchini yaliyotaifishwa wakati wa Azimio la Arusha. Baadhi ya mashamba hayo yaligawiwa kwa mashirika na taasisi za Umma kwa ajili ya kuyaendeleza hususan kwa kilimo cha kahawa na mkonge.

Hata hivyo, baadhi ya mashamba hayo yamebadilishiwa matumizi na yamekuwa yakitumiwa na wananchi kwa matumizi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii ikiwemo makazi, shule, zahanati, hospitali na kadhalika. Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri mbalimbali nchini, imeendelea kuyakagua, kuyaandalia mipango ya matumizi ya ardhi na kupima upya baadhi ya mashamba hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mashamba ambayo Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri imeyaandalia mpano wa matumizi ya ardhi ni pamoja na Kihuhwi Estate, Sagulas Estate, Lewa Estate, Bombwera Estate, Geiglitza Azimio, Kilapula pamoja na Kibaranga yote ya Mkoa wa Tanga. Mashamba mengine ni New Msovero Farm, Mvumi Farms/Estate Kilosa pamoja na Luipa Estate yaliyopo Mkoani Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi jukumu la kuandaa mipango ya matumizi ya mashamba hayo ni la Halmashauri husika yalipo mashamba hayo. Hivyo, ninaagiza Halmashauri zote nchini kuendelea kukagua mashamba yaliyotaifishwa wakati wa Azimio la Arusha ili yaandaliwe mipango ya matumizi ya ardhi na kupimwa.

Aidha, natoa rai kwa Halmashauri zote nchini kuhakikisha zinatenga bajeti kwa ajili ya kupanga na kupima mashamba husika ili yaweze kutumika kwa tija kulingana na mahitaji halisi ya sasa.