Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 78 2019-04-15

Name

Kiza Hussein Mayeye

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. KIZA H. MAYEYE aliuliza:-

Serikali imekuwa ikiwapandisha madaraja walimu lakini haitoi malipo stahiki kwa madaraja hayo mapya kwa kipindi kirefu tangu walipopandishwa madaraja yao:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba walimu wanapata stahiki zao mara wanapopandishwa madaraja?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiza Hussein Mayeye, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilisitisha kupandisha walimu na watumishi wengine madaraja katika mwaka wa fedha 2015/2016 na 2016/2017 kutokana na uhakiki wa watumishi uliohusisha uhalali wa vyeti, elimu na ngazi za mishahara. Lengo la uhakiki ilikuwa ni kuhakikisha kuwa Serikali inabaki na watumishi wenye sifa na wanaostahili kulipwa mishahara. Kutokana na sababu hiyo, ni kweli wapo watumishi ambao walipandishwa madaraja ambao hawajalipwa mishahara mipya, wapo waliopata mishahara mipya na baadaye kuondolewa na wapo ambao hawakupandishwa kabisa pamoja na kwamba walikuwa na sifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kurekebisha changamoto hizo, Serikali ilitoa maelekezo kuanzia Novemba, 2017 kwa waajiri wote wakiwemo Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhuisha barua za kupandisha madaraja watumishi hao ili waweze kulipwa stahiki zao. Aidha, kwa wale ambao walikuwa na barua lakini taarifa zao zilikuwa hazijaingizwa kwenye mfumo, waajiri walielekezwa kuhuisha barua zao kuanzia tarehe 1 Aprili, 2018 ili waanze kulipwa stahiki zao. Serikali itaendelea kuweka kipaumbele na kutenga bajeti kwa ajili ya kuhakikisha watumishi wenye sifa na kupanda madaraja wanalipwa stahiki zao.