Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 10 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 80 2019-04-15

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-

Halmshauri ya Longido inatakiwa kuwa na watumishi 1,660 wa kada mbalimbali lakini kwa sasa wapo 1atumishi 1,117 tu, hivyo, kuna upungufu wa watumishi 543 na wengi wao ni Watendaji wa Vijiji, Kata, Madereva na Makatibu Muhtasi:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa vibali vya kuajiri watumishi wanaohitajika ili kuondoa upungufu uliopo?

(b) Je, ni lini Serikali itatoa vibali vya kuwathibitisha maafisa wanaokaimu wenye sifa za kuajiriwa?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Mbunge wa Longido, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inakiri kuwepo kwa tatizo la upungufu wa watumishi kwa waajiri mbalimbali hapa nchini na siyo kwa Halmashaui ya Wilaya ya Longido pekee. Upungufu huu umesababishwa kwa kiasi kikubwa sana na zoezi la kuwaondoa katika Utumishi wa Umma watumishi waliobainika kutumia vyeti vya kughushi katika ajira zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na upungufu wa watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido, Serikali imetoa kibali cha ajira mbadala nafasi tano (5). Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Longido itapatiwa nafasi za Walimu na Fundi Sanifu Maabara kutoka kwenye mgawo wa nafasi 4,549 za Ajira Mbadala za Walimu ambazo mchakato wake unaendelea chini ya Ofisi ya Rais - TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine, Halmashauri ya Wilaya ya Longido imetengewa jumla ya nafasi 177 za kada mbalimbali zikiwemo Watendaji wa Vijiji, Kata, Madereva na Makatibu Muhtasi katika mwaka wa fedha ule 2018/2019. Katika kuhakikisha suala la upungufu wa watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Longido linapatiwa ufumbuzi wa kudumu, Serikali itaendelea kutenga nafasi za ajira mpya pamoja na kutoa vibali vya Ajira Mbadala kwa kada za kipaumbele katika mwaka wa fedha 2019/2020 na kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika sehemu (b) ya swali la Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Mbunge wa Longido, naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba watumishi wa umma wanaothibitishwa katika nafasi za uongozi kwa maana ya madaraka ni wale walioteuliwa rasmi katika nafasi hizo baada ya taratibu za upekuzi kukamilika. Aidha, hakuna utaratibu wa kuthibitisha watumishi wa umma wanaokaimu nafasi za uongozi kwa maana ya madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hufanya upekuzi kwa watumishi wa umma wanaokaimu nafasi za madaraka ili kubaini iwapo wanafaa au la. Uamuzi iwapo mtumishi husika anafaa kuteuliwa kwenye nafasi anayokaimu hutegemea na matokeo na upekuzi. Hivyo, pamoja na kuwa na sifa za kitaaluma, Serikali hailazimiki kumthibitisha mtumishi iwapo anakosa vigezo vingine vya uongozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa rai kwa watumishi wa umma wote nchini wanaokaimu nafasi za uongozi wafanye kazi kwa bidii, weledi, umahiri, uzalendo kwa kuzingatia maadili ya kazi ili waweze kukidhi vigezo vya kuteuliwa na kisha waweze kuthibitishwa kwenye nafasi za uongozi ambazo ni madaraka wanazoteuliwa kuzishika. Ahsante.