Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 15 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 124 2019-04-24

Name

Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. JOSEPH L. HAULE aliuliza:-

Jimbo la Mikumi lina uhaba mkubwa wa Vituo vya Afya na hata pale ambapo kuna Kituo, basi dawa na Wataalamu ni tatizo:-

Je, Serikali imejipanga vipi kutatua tatizo hilo sugu la uhaba wa Vituo vya Afya na dawa?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa ina jumla ya vituo vya afya vitano. Kati ya vituo hivyo viwili vipo katika Jimbo la Mikumi ambavyo ni Kituo cha Afya Kidodi na Ulaya. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Kituo cha Afya cha Kidodi kilipatiwa jumla ya shilingi milioni 400 za ukarabati na kwa sasa kinatoa huduma za upasuaji kwa akinamama wajawazito. Vilevile Kituo cha Afya Kidodi kimepatiwa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 95 ili kukiwezesha kuanza kutoa huduma. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019 zahanati ya Mikumi ilipewa jumla ya shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuongeza majengo ili iweze kukidhi vigezo vya kupandishwa hadhi kwa Kituo cha Afya na mpaka sasa kazi ya ujenzi inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri kwa kushirikiana na wananchi wa Kata ya Malolo inaendelea na ujenzi wa Kituo cha Afya Malolo kwa kutumia mapato ya ndani ambapo ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje, maabara, jengo la upasuaji na wodi ya wazazi yapo katika hatua ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 1.07 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vitendanishi. Vilevile katika mwaka wa fedha 2018/2019 hadi Februari, 2019 Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa imepokea shilingi milini 849 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vitendanishi ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa kwa mwaka wa fedha 2016/2017 na 2017/2018 Serikali iliajiri jumla ya wataalam wa afya 8,238 ambapo Halmashauri ya Kilosa ilipata jumla ya wataalam 42 wa kada mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kujenga vituo vya afya kote nchini pamoja na kuajiri wataalam wa afya kulinga na upatikanaji wa rasilimali fedha.