Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 2 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 16 2020-01-29

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-

Katika eneo linalopatikana gesi aina ya carbondioxide (CO2) kwenye Jimbo la Busekelo, Kijiji cha Mpata kuna visima ambavyo ni hatari kwa binadamu na viumbe hai wengine kwani huwa wanakufa wakivuta hewa ya sehemu hiyo:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kunusuru maisha ya binadamu na viumbe katika eneo hilo?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busekelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa katika Jimbo la Busekelo, katika Kijiji cha Mpata kuna visima vya gesi ya ukaa (Carbondioxide) vinavyomilikiwa na Kampuni ya Tanzania Oxygen Limited. Kampuni hiyo inamiliki leseni mbili za uchimbaji wa gesi ya ukaa ambazo ni ML 139/2002 iliyotolewa tarehe 17/11/2002 na ML 379/2009 iliyotolewa tarehe 21/08/2009. Kisima cha Mpata Kipo katika leseni Na. ML 139/2002.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la Mpata kuna visima viwili. Kisima kimoja kilichimbwa na kimefunikwa madhubuti na Kampuni ya Tanzania Oxygen Limited ambayo inavuna gesi ya ukaa. Kisima cha pili kimetokana na nguvu za asili zilizosababishwa na mlipuko wa volkano na hivyo kupelekea uwepo wa kisima cha asili. Kutokana na uwepo wa kisima hicho kilichotokana na njia ya asili, tafiti za awali zinatoa tahadhari ya kisima hicho kikifunikwa kinaweza kutoa gesi hiyo kupitia njia nyingine na hivyo kuleta madhara yasiyotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo hayo ili kudhibiti athari inayoweza kutokea. Hatua za udhibiti zilizochukuliwa na Serikali kwa kushirikiana na TOL ni pamoja na kuweka vizuizi madhubuti, uzio na ulinzi wakati wote kwa watu na wanyama ili wasiweze kufika katika eneo la kisima sambamba na kuweka mabango ya tahadhari katika eneo hilo. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na TOL inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu hatari za gesi ya ukaa katika maeneo yanayozalishwa gesi hiyo. Ahsante.