Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 4 Water and Irrigation Wizara ya Maji 45 2020-01-31

Name

Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FELISTER A. BURA aliuliza:-

Kutokana na Serikali kuhamia Dodoma, mahitaji ya maji safi na salama yamekuwa makubwa na kwa sasa mgao wa maji kwa wakazi wa Dodoma umeshaanza:-

Je, Serikali ina mpango gani mahsusi wa kuhakikisha wakazi wa Dodoma wanapata maji safi na salama?

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, chanzo kikubwa cha uzalishaji maji kwa matumizi ya wakazi wa Jiji la Dodoma ni visima virefu vilivyochimbwa katika Bonde la Makutopora eneo la Mzakwe. Kuna jumla ya visima vya uzalishaji maji 24 na visima vitano vya kuchunguza mwenendo wa maji ardhini (observation boreholes) vimechimbwa katika bonde hilo. Uwezo wa visima vilivyopo Mzakwe kwa sasa pamoja na uwezo wa usafirishaji wa maji ni mita za ujazo 61,500 kwa siku.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha huduma ya maji inakuwa ya uhakika, Serikali kupitia Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Jijini Dodoma, imeongeza chanzo kingine cha maji eneo la Ihumwa chenye uwezo wa kuzalisha maji mita za ujazo 2,773 kwa siku. Chanzo hiki kina visima nane na kinahudumia Mji wa Serikali uliopo Mtumba pamoja na Kijiji cha Ihumwa.

Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuboresha huduma ya maji, kwa mpango wa muda mfupi Serikali inaendelea na utafiti wa maji chini ya ardhi na uchimbaji wa visima virefu katika Mitaa ya Ntyuka, Michese na Nala na uendeshaji wa visima nane katika Mji wa Chamwino. Mpango wa muda wa kati wa ujenzi wa Bwawa la Maji la Farkwa litakalotumika kama chanzo cha nyongeza cha majisafi katika Jiji la Dodoma.