Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 5 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 57 2020-02-03

Name

Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. JOSEPH L. HAULE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafuta umiliki wa mashamba pori ya muda mrefu ya Mauzi Estate, Miyombo Estate, Sumagro Estate Kisanga Estate (Lyori Estate) yaliyopo kwenye kata za Tindiga, Masanze, Kilangali na Kisanga na kuyagawa kwa wananchi wanyonge ili waweze kupata maeneo hayo wanayoyahitaji sana ili kufanya shughuli zao mbalimbali za kujiletea maendeleo?

Name

William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Answer

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kuchukua hatua dhidi ya wamiliki wote wa ardhi nchini ambao wameendelea kukiuka masharti ya kumiliki ardhi ikiwemo kutoendeleza ardhi kwa mujibu wa sheria na taratibu; kuendeleza ardhi kinyume na masharti ya umiliki; na kutolipa kodi ya pango la ardhi.

Kwa upande wa mashamba, katika kipindi cha kuanzia Disemba, 2015 mpaka sasa, jumla ya milki za mashamba 45 zimebatilishwa katika maeneo mbalimbali nchini. Kwa Mkoa wa Morogoro, jumla ya mashamba 15 yamebatilishwa ambapo mashamba 10 kati ya hayo yapo katika Wilaya ya Kilosa anapotoka Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu iliunda timu ya kupitia mashamba yote yaliyobatilishwa katika Mkoa wa Morogoro pamoja na kukagua mashamba yenye sifa za kubatilishwa. Mashamba ya Mauzi Estates, Sumagro Estates, Kisanga Estates na Miyombo ni miongoni mwa mashamba ambayo timu yangu iliweza kuyakagua na hatua za ubatilisho wa milki zinaendelea. Jumla ya mashamba yaliyokaguliwa na kupendekezwa kubatilishwa ndani ya Mkoa wa Morogoro ni 23 na yote yapo katika Wilaya ya Kilosa. Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa imeelekezwa kufanya taratibu za ubatilisho kwa mashamba hayo haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa ambazo zimebaini kuwepo kwa mashamba yasiyoendelezwa katika maeneo yao, kuwasilisha Wizarani mapendekezo ya kubatilisha milki za mashamba husika ili taratibu za kuyabatilisha zikamilishwe kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi (Sura113).