Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 3 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 31 2019-09-05

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Primary Question

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI (K.n.y. MHE. ENG. RAMO M. MAKANI) aliuliza:-

Utekelezaji wa Mpango wa Kaya Maskini katika Jimbo la Tunduru Kaskazini una changamoto nyingi sana zinazolalamikiwa na Wananchi:-

Je, Serikali itachukua hatua zipi za makusudi kurekebisha kasoro hizo ili wananchi wapate kunufaika vema zaidi na huduma za Mfuko huo?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala bora, naomba kujibu swali la Eng. Ramo Matala Makani kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingawa Mheshimiwa Eng. Makani hakutaja waziwazi changamoto za utekelezaji wa mpango kwenye Jimbo lake, Serikali kupitia TASAF, changamoto kubwa ambayo Mpango unakumbana nao ni kilio kutoka kwa baadhi ya wananchi maskini ambao hawajafikiwa na huduma za Mpango huo kwenye Vijiji/ Mitaa/Shehia takribani 5,693 ambavyo havikufikiwa katika Awamu ya Kwanza ya Mpango huu wa kunusuru kaya maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Makani na Wabunge wengine kwamba utaratibu umeshaandaliwa wa kuweza kufika kwenye Vijiji/ Mitaa/Shehia hizo mara tu baada ya mpango kuanza utekelezaji. Katika awamu hii, TASAF imejipanga vizuri kuhakikisha kuwa yale malalamiko ya upendeleo, ubaguzi na kuachwa kwa watu maskini kuandikishwa kwenye Mpango huu hayajirudii na mifumo ya kielekroniki itatumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge na viongozi wote kwamba muda utakapofika wahakikishe wanalisimamia vizuri zoezi la utambuzi wa walengwa ili wale wanaostahili basi waweze kuwa wameandikishwa kwenye mpango huu. Hatua kali zitachukuliwa kwa viongozi na watumishi katika ngazi zote ambao katika maeneo yao watabainika kuwepo watu au kaya zisizo na vigezo kwenye Awamu ya Pili ya Mpango huu wa Kunusuru Kaya Maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ni malalamiko ya walengwa kuhusu makato ya fedha kipindi cha malipo. Suala hili walengwa wanaendelea kuelemishwa kwa nini makato yanatokea. Sababu ya kukatwa fedha zao ni kutokana na kutotimiza masharti ya kupokea ruzuku hasa kwa kaya zenye watoto walio shuleni halafu hawaendi shule na wale wanaotakiwa kuhudhuria kliniki ambao ni watoto wenye umri wa miaka mitano na hawafanyi hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, endapo kaya itashindwa kutimiza masharti ya kutimiza watoto hao kutohudhuria shuleni au kutopeleka watoto kliniki fedha hizo zinakatwa kama adhabu. Nimuombe Mheshimiwa Makani na Wabunge wengine wote, mnapoenda kwenye ziara katika Majimbo yenu ndugu zangu tusaidiane kutoa elimu hii ili kuepusha malalamiko ambayo sio ya lazima. Ahsante.