Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 54 2019-09-06

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa Hatimiliki kwa Vijiji vilivyopimwa na kusajiliwa ambavyo bado havijapewa Hati?

Name

William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Answer

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya mwaka 2001, vijiji vilikuwa vinapimwa na kupatiwa Hatimiliki ambayo ilikuwa inatolewa kwa Halmashauri za Vijiji kwa kuzingatia Sheria ya Ardhi ya Mwaka 1923. Baada ya Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na.5 ya Mwaka 1999 kutungwa na kuanza kutumika mwezi Mei, 2001, ilielekeza kuwa vijiji vilivyotangazwa na kusajiliwa vitapimwa na kupatiwa cheti cha ardhi ya kijiji badala ya Hatimiliki iliyokuwa inatolewa hapo awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cheti hicho hutolewa kwa mujibu wa Kifungu cha 7(7) cha Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 ya Mwaka 1999 ili kuipatia Halmashauri ya Kijiji majukumu ya kusimamia ardhi pamoja na kuwapatia haki ya ukaaji na utumiaji wa ardhi ya kijiji wanakijiji wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Cheti cha Ardhi ya Kijiji kinathibitisha mamlaka ya Halmashauri ya Kijiji kusimamia ardhi ya kijiji tofauti na Hatimiliki ambayo ilimaanisha Halmashauri ya Kijiji kumiliki ardhi ya kijiji na hivyo kuwanyima fursa wanakijiji kumiliki ardhi kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, cheti hiki hutolewa na Kamishina wa Ardhi kwa kijiji husika kikiwa kinaonyesha mipaka ya ardhi iliyowekwa na kukubaliwa na pande zote zinazopakana na kijiji husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi Julai, 2019 Wizara imewezesha uandaaji na utoaji wa vyeti vya ardhi ya vijiji 11,165 kati ya vijiji 12,545 vilivyosajiliwa. Serikali inaendelea na utaratibu wa utatuzi wa migogoro ya mipaka ya vijiji kwa maeneo ambayo bado hayajapatiwa vyeti ambayo haizidi asilimia 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa Halmashauri zote nchini kuhakikisha kuwa zinashirikiana na wadau wengine katika kusimamia utatuzi wa migogoro ya mipaka baina ya vijiji kwa njia ya maridhiano ili taratibu za upimaji na utoaji wa vyeti wa vijiji ufanyike.