Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 1 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 7 2021-08-31

Name

Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Primary Question

MHE. KAVEJURU A. FELIX Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Standard Gauge Railways kutoka Tabora kwenda Kigoma?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Aliadory Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kupitia Shirika la Reli Tanzania (TRC) inaendelea na ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha Standard Gauge kwa awamu ya kwanza kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza yenye urefu wa kilomita 1,219. Kutokana na gharama kubwa za ujenzi na ili kurahisisha ujenzi, awamu ya kwanza inajengwa katika vipande vitano ambavyo ni Dar es Salaam – Morogoro (kilometa 300), Morogoro – Makutupora (kilometa 422), Makutupora – Tabora (kilometa 368), Tabora – Isaka (kilometa 165) na Isaka – Mwanza (kilometa 341).

Mheshimiwa Spika, ujenzi katika vipande vitatu vya Dar es Salaam – Morogoro (kilometa 300), Morogoro – Makutupora (kilometa 422) na Mwanza – Isaka (kilometa 341) unaendelea na Serikali inakamilisha taratibu za manunuzi ya makandarasi kwa ajili ya ujenzi wa reli ya Standard Gauge kwa vipande vya Makutupora – Tabora (kilometa 368) na Tabora – Isaka (kilometa 165).

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa reli ya Tabora – Kigoma (kilometa 411) Serikali imemuajiri Mshauri Elekezi wa Kampuni ya COWI kwa ajili ya kufanya upembuzi na usanifu wa awali wa ujenzi wa reli hii kwa kiwango cha Standard Gauge. Kazi hii inaendelea na inatarajiwa kukamilika Septemba, 2021.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Serikali inaendelea kutafuta fedha kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo kwa ajili ya kupata mkopo wenye masharti nafuu kwa lengo la kukamilisha ujenzi wa mtandao mzima wa reli kwa kiwango cha Standard Gauge ikiwemo reli ya Tabora – Kigoma (kilometa 411), Kaliua – Mpanda – Karema (kilometa 316.7).

Mheshimiwa Spika, ahsante.