Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 19 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 161 2016-05-13

Name

Elias John Kwandikwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ushetu

Primary Question

MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Serikali imekuwa ikitumia waajiriwa wa muda (vibarua) ambao hawana ujuzi, uadilifu wala taaluma ya uhifadhi:-
(a) Je, ni vibarua wangapi walitumiwa katika Hifadhi ya Kigosi kwa kipindi cha miaka mitano (2010-2015)?
(b) Je, Serikali ilikuwa imetenga kiasi gani cha fedha na ni kiasi gani kililipwa kwa vibarua hao?

Name

Prof. Jumanne Abdallah Maghembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NAUTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya shughuli ambazo hazihitaji ujuzi mahsusi kama usafishaji wa ofisi, kufyeka barabara na mipaka ya hifadhi. Kazi hizo hutolewa kwa wananchi waishio kando ya hifadhi ikiwa ni njia mojawapo ya kuwapatia kipato na kukuza mahusiano mema kati Serikali na wananchi hivyo kuwapa faida za moja kwa moja za kiuchumi kutokana na kuwepo jirani na hifadhi. Aidha, wapo vibarua ambao hufanya kazi zinazohitaji elimu na ujuzi mahsusi wa wastani kama vile ukatibu muhtasi na udereva ambao huhitaji kuwa na vyeti na leseni zinazoruhusu kufanya kazi hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida hakuna kibarua anayefanya kazi za kiuhifadhi moja kwa moja kwani kazi hizo zinahitaji taaluma, ujuzi na uzoefu wa masuala ya uhifadhi wa wanyamapori katika viwango vinavyokubalika na taaluma yenyewe. Ajira za vibarua hutolewa kulingana na mahitaji ya ofisi, hivyo wanaokidhi vigezo hupewa mikataba ya ajira kwa kipindi kisichozidi miezi mitatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Pori la Kigosi kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2010 - 2015 jumla ya vibarua 240 walifanya kazi za muda kama kufyeka barabara na mipaka na kusaidia kufanya usafi wa kambi na miradi ya maendeleo kama vile ujenzi wa nyumba, ukarabati wa majengo kwa kushirikiana na Askari wa Wanyamapori.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi hicho jumla ya shilingi milioni 27.8 zilitumika katika kuwalipa vibarua hao. Aidha, kampuni zinazoendesha shughuli za utalii katika mapori huajiri vibarua kwa ajili ya shughuli zao.