Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 4 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 40 2016-01-29

Name

Munde Abdallah Tambwe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MUNDE T. ABDALLAH aliuliza:-
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora inakabiliwa na kero mbalimbali kama vile ukosefu wa madaktari bingwa wa watoto, akina mama, mifupa, na kadhalika; ukosefu wa vifaa muhimu kama vile ECG machine, CT-Scan, MRI machine, ukosefu wa huduma za ICU pamoja na kwamba lipo jengo zuri lakini halina vifaa vya huduma za dharura:-
Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kutatua kero hizi zinazokabili hospitali hii kwa muda mrefu?

Name

Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Munde Tambwe Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua changamoto ya Madaktari Bingwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora, Serikali imewapeleka masomoni Madaktari Bingwa wawili akiwemo Daktari wa Upasuaji na Daktari wa Watoto. Aidha, Mkoa katika bajeti ya mwaka 2015/2016 imeomba kibali cha kuajiri Madaktari Bingwa wanne ili kuboresha utoaji wa huduma ya afya. Kwa sasa hospitali hiyo inatumia Madaktari Bingwa watano kutoka China wanaojitolea ambao wamebobea katika maeneo ya tiba, upasuaji, huduma za uzazi, watoto na huduma ya masikio, pua na koo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa vifaa, Serikali imepanga kusimika vifaa vya kuangalia mwenendo wa afya ya wagonjwa (patient monitor), vifaa vya uchunguzi wa tiba vikiwemo ECG, CTG, Pulse Oxymeter na Oxygen Concentrator katika hospitali zote za ngazi ya mkoa ikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora. Mpango huu unatarajiwa kuanza mwaka huu wa fedha 2015/2016 na unahisaniwa na Uholanzi kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania. Aidha, Serikali ina mpango wa kuweka huduma ya MRI kwenye Hospitali za Rufaa za Kanda na Taifa ambapo kwa mwaka 2015/2016, huduma hii itasimikwa katika Hospitali ya Kanda ya Bugando ambayo inahudumia pia wakazi wa Mkoa wa Tabora.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Mkoa wa Tabora umeingia makubaliano na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF), ili kuweza kukopeshwa vifaa muhimu, hususan kwa ajili ya huduma za dharura (ICU).