Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 4 Finance and Planning Ofisi ya Rais TAMISEMI. 41 2016-01-29

Name

Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-
Sera Mpya ya Elimu ya mwaka 2014 inatambua upatikanaji wa elimu ya msingi bure; lakini Serikali imeshindwa kupeleka ruzuku ya shilingi 10,000 kwa kila mwanafunzi wa shule za msingi za umma na shilingi 25,000/= kwa kila mwanafunzi wa shule za sekondari za umma:-
Je, Serikali inaweza kuweka mchanganuo wa jinsi gani itakavyoweza kutekeleza Sera ya Elimu ya mwaka 2014 kwa kutoa elimu bure bila kuathiri ubora wa elimu?

Name

Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malopo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli fedha za uendeshaji wa elimu (capitation) zikiwemo shilingi 10,000/= kwa wanafunzi wa shule ya msingi na shilingi 25,000/= kwa wanafunzi wa sekondari zilikuwa hazipelekwi kwa ukamilifu. Kwa sasa Serikali imeamua kuanzia Januri, 2016 wanafunzi wote walioandikishwa darasa la kwanza na wale walioandikishwa kidato cha kwanza pamoja na wale wanaoendelea na shule gharama zilizokuwa zinagharimiwa na wazazi au walezi kwa kulipia ada na michango mbalimbali sasa zitalipwa na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanzia Serikali imetenga shilingi bilioni 131.4 ikiwa ni fedha za ruzuku ya uendeshaji wa shule, chakula, mitihani na fidia ya ada. Fedha hizo zitapelekwa moja kwa moja shuleni kutoka Hazina kwa wastani wa shilingi bilioni 18.77 kila mwezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizo zinahusisha shilingi 10,000/= kwa wanafunzi wa shule ya msingi kwa mwaka, shilingi 25,000/= kwa mwanafunzi wa sekondari kwa mwaka, shilingi 1,500/= kwa kila mwanafunzi kwa shule za msingi na sekondari kwa ajili ya chakula, fidia ya ada ya shilingi 20,000/= kwa wanafunzi wa kutwa na shilingi 70,000/= kwa wanafunzi wa bweni kidato cha kwanza hadi cha nne kwa mwaka. Tayari Serikali imeshapeleka shilingi bilioni 18.77 kwa mwezi Januari, 2016.