Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 20 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 170 2016-05-16

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Katika Halmashauri ya Mbeya kuna mradi wa uchimbaji wa madini unaotarajiwa kuanza kwenye eneo la Mlima Songwe, lakini pia kuna mradi mwingine mkubwa wa joto ardhi kwenye Kata za Swaya, Ijombe na Bonde la Songwe.
(a)Je, kwa nini Serikali Kuu haihusishi Halmashauri ya Mbeya katika mradi hiyo ili elimu iweze kutolewa kwa wananchi?
(b)Je, wananchi wa Jimbo la Mbeya Vijijini watanufaika vipi na miradi hiyo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kifungu Namba 95(1)(b) cha Sheria Sheria ya Madini Namba14 ya 2010, kabla ya kuanza utafutaji na uchimbaji wa madini, mmiliki wa leseni husika hutakiwa kupata kibali cha kumruhusu kuingia na kushughulika na utafutaji na uchimbaji wa madini kutoka kwenye Halmashauri za zilaya pamoja na mkoa. Kampuni za Cradle Resources Ltd/RECB Co. Ltd. ilipewa leseni tatu za uchimbaji wakati wa madini ya niobium. Leseni hizo ni ML 237, 238 na 239 zilitolewa mwaka 2006 zenye jumla ya ukubwa wa eneo la kilometa za mraba 22.06. Kwa sasa kampuni hiyo inakamilisha maandalizi kabla ya kuanza kwa ujenzi wa mgodi huo ifikapo mwaka 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa utafiti wa madini hayo ya niobium kampuni ya Cradle Resources Ltd/RECB Co. Ltd. inayomiliki leseni ilijitambulisha kwa uongozi wa mkoa wa Mbeya ikiwa ni pamoja na Gereza la Songwe ambapo mradi huo upo. Aidha, kampuni hiyo hivi sasa iko kwenye mazungumzo ya Gereza la Songwe pamoja na Wizara ya Mambo ya Ndani kuona namna ya kulihamisha Gereza hilo kabla ya kuanza uchimbaji kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa niobium utakuwa na faida kubwa kwa uchumi wa viwanda ikizingatiwa kwamba Serikali inajikita katika kufufua na kukuza viwanda nchini. Miongoni mwa matumizi ya madini haya ni kutumika kama alloy kwenye chuma kwa kuboresha uimara wake. Vilevile madini hayo hutumika katika kutengeneza mabomba mathalani mabomba ya kusafirisha gesi asilia. Matumizi mengine ya madini haya ni matengenezo ya sumaku pamoja na utengenezaji wa injini za ndege na rocket.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Tanzania Geothermal Development Company Limited (TGDC) ni kampuni tanzu ya Shirika la Umeme nchini (TANESCO) ambayo imepewa dhamana ya kusimammia miradi ya kufua umeme wa joto ardhi katika Ziwa Ngozi lililopo kati ya Mbeya Vijijini. Mradi huu pia utazalisha umeme wa megawati 20 kwa kuanzia na baadaye utaweza kuzalisha megawati 100. Shughuli za utafiti wa mradi huu zilianza mwaka 2015 na zinatarajiwa kukamilika mwaka 2018 kwa kuzalisha umeme wa megawati 20. Mwezi Agosti 2015, kampuni ya TGDC iliendesha mafunzo kwa viongozi wa Mkoa, Wakuu wa Wilaya, watendaji wa Kata na vijiji wa Mbeya yaliyolenga kuwajengea uelewa wananchi hao. Aidha, mafunzo kama hayo yalitolewa kwa njia ya mihadara kwa wananchi wa Vijiji vya Ijombe, Mwakibete, Nanyara na Swaya vinavyozunguka maeneo yanayofanyiwa utafiti wa joto ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na joto ardhi kutumika kuzalisha umeme manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi wanaozunguka eneo la mradi ni pamoja na kutumia maji ya moto majumbani lakini pia katika vitalu vya kilimo. Kadhalika itatumika katika kufugia samaki, kukausha mazao, kujenga mabwawa ya kuogelea na kwa matumizi mengine ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla miradi ya uwekezaji hunufaisha wananchi wa eneo husika katika ukuaji wa shughuli za kiuchumi na ajira. Miradi hii miwili itakapotekelezwa wananchi wa Halmashauri ya Mbeya Vijijini, Rungwe, Mbeya pamoja na Watanzania wote watanufaika kwa kupata ajira, ushuru pamoja na tozo mbalimbali pamoja na huduma za jamii.