Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 24 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 205 2016-05-20

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUSAN L. KIWANGA (K.n.y. MHE. DEVOTHA M. MINJA) aliuliza:-
Askari wa Jeshi la Polisi na Magereza wanaishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi ikilinganishwa na kazi zao wanazofanya kwa jamii:-
Je, Serikali ina mpango gani kuwaboreshea makazi?

Name

Charles Muhangwa Kitwanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Misungwi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama yalivyowahi kujibiwa maswali kadhaa ndani ya Bunge lako Tukufu kuhusu askari kuboreshewa makazi, Serikali inafahamu kuwa lipo tatizo la baadhi ya askari wa Jeshi la Magereza na Polisi kuishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi. Namwona rafiki yangu hapa anashusha kichwa ananyanyua. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na tatizo hilo, Serikali imeendelea na mpango wake wa kuzifanyia ukarabati mkubwa baadhi ya nyumba na kwenye baadhi ya magereza kujenga nyumba na vilevile kuendelea kuona mahitaji ya nyumba na hivi sasa ni nyumba 14,500 wakati zilizopo ni 4,221 hivyo kuwepo upungufu wa nyumba 10,279 ambao unalazimisha baadhi ya askari kuishi nje ya Kambi za Jeshi la Magereza. Hata hivyo, kasi ya utekelezaji wa mpango huu umekuwa ni mdogo kutokana na kuathiriwa na ufinyu wa bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupande wa Jeshi la Polisi, Serikali inakusudia kujenga nyumba 4,136 katika mikoa 17 ya Tanzania Bara na Zanzibar kama nilivyozungumza kwenye bajeti yetu. Aidha, Serikali itaendelea kutatua changamoto ya uhaba wa nyumba kwa kutumia njia mbadala ikiwemo mikopo yenye riba nafuu, Miradi Shirikishi (PPP) na kwa kutumia fedha za bajeti ya Serikali kadiri hali ya uchumi itakavyokuwa ikiimarika. Mkakati huu utakwenda sambamba na mipango. Nirudie tena, mkakati huu utakwenda sambamba na mipango ya maendeleo ya Serikali ikilenga kufikia idadi ya nyumba za makazi kwa askari wote waliopo sasa na watakaoajiriwa baadaye.