Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 47 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 400 2016-06-21

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Mji Mdogo wa Mbalizi uliomo kwenye Halmashauri ya Mbeya ni kati ya miji inayokua kwa kasi sana lakini inakosa miundombinu muhimu na uhaba na maji pia.
(a) Je, ni lini Mji huo utapewa hadhi ya kuwa Halmashauri ya Mji?
(b) Je, ni lini Serikali itatatua tatizo kubwa la maji kwenye Mji huo?
(c)Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya kwenye kata zilizo ndani ya Mji wa Mbalizi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, uanzishaji wa Halmashauri za Miji nchini unazingatia Sheria ya Serikali za Mitaa Sura 288 (Mamlaka za Miji) ambayo imeainisha taratibu na vigezo vinavyopaswa kuzingatiwa. Hivyo, nashauri pendekezo hili lijadiliwe kwanza katika vikao vya Kamati za Maendelo ya Kata, Baraza la Madiwani na Kamati ya Ushauri ya Mkoa. Endapo vikao hivyo vitaridhia, Ofisi ya Rais - TAMISEMI haitasita kuyafanyia kazi mapendekezo hayo ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji Mdogo wa Mbalizi unapata maji kutoka chanzo cha Ilunga chenye uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 3,024 za maji kwa siku pamoja na visima kumi vya maji ambavyo vina uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 6,300 kwa siku. Mji wa Mbalizi umeingizwa katika Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Maji awamu ya pili ambapo Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa kushirikiana na Halmashauri inakusudia kuunganisha Mji huo na Mamlaka ya Maji Mkoa wa Mbeya ili kupata maji yatakayotosheleza mahitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mji wa Mbalizi wanapata huduma za afya kupitia Hospitali Teule ya Mbalizi pamoja na Hospitali ya Jeshi la Wananchi ambako Halmashauri imeendelea kutoa mchango wa dawa na watumishi. Hivyo, katika mwaka wa fedha 2016/2017, kipaumbele kimewekwa katika kukamilisha ujenzi wa zahanati nane ndani ya Halmashauri zilizoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi.