Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 48 Works, Transport and Communication Ofisi ya Rais TAMISEMI. 409 2016-06-22

Name

Eng. Joel Makanyaga Mwaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chilonwa

Primary Question

MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:-
Barabara inayounganisha vijiji vya Msanga na Kawawa ni muhimu sana kiuchumi kwa kata ya Msanga na Wilaya ya Chamwino na pia kuna mazao mengi ya uhakika kutoka Kawawa na vitongoji vyake, lakini barabara hiyo ni korofi sana kwa sababu ya mbuga iliyoko kati ya vijiji hivyo viwili na zaidi, daraja kubwa lililopo limevunjika kabisa kiasi kwamba halipitiki kabisa wakati wa mvua na wakati wa kiangazi hupitika kwa taabu sana.
Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha barabara hiyo na kulijenga daraja husika ili kuboresha mawasiliano ya vijiji hivi viwili na masuala ya usafirishaji?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joel Mwaka Makanyaga, Mbunge wa Jimbo la Chilonwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali katika mwaka wa fedha 2015/2016 imetenga shilingi milioni 46.3 kwa ajili ya kujenga kivuko (box culvert), kuichonga barabara kwa urefu wa kilometa tano na kuiwekea changarawe sehemu korofi yenye urefu wa kilometa nne. Aidha, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017, barabara hii imeombewa shilingi milioni 130 kwa ajili ya ukarabati ili kuifanya ipitike wakati wote.