Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 5 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 58 2016-02-01

Name

Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Kigoma Mjini

Primary Question

MHE. KABWE Z. R. ZITTO aliuliza:-
Mwaka 2013 Serikali iliuza hatifungani ya thamani ya Dola za Kimarekani milioni mia sita (USD 600m) kupitia benki ya Standard yenye tawi hapa nchini (Stanbic); Shirika la Corruption Watch la Uingereza kwa kutumia vyanzo kama IMF imeonesha kwamba hatifungani hiyo imeipa Serikali ya Tanzania hasara ya Dola za Kimarekani milioni themanini (USD) 80.m) na Serikali imelipwa faini Dola za Kimarekani milioni sita (USD Six Million) tu.
Je, kwa nini Serikali haiichukulii hatua Stanbic Bank ili walipe faini zaidi?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabwe Ruyagwa Zitto, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika mahitaji yaliyofanywa na serious fraud office ya Uingereza dhidi ya Standard Bank Group, Serious Fraud Office ilitambua kiasi cha Dola za Kimarekani milioni sita, sawa na asilimia moja ya mkopo ambao Tanzania haikupaswa kutozwa. Tozo (arrangement fee) iliyotakiwa kulipwa kwa Standard Bank Group ni asilimia 1.4. Badala yake tozo iliyoingizwa kwenye mkataba ni aslimia 2.4, na ilithibitika kwamba tozo ya asilimia moja ya ziada haikuwa halali.
Katika hukumu iliyotolewa na Mahakama huko Uingereza Standard Bank Group iliamriwa kulipa faini ya Dola za Kimarekani milioni thelathini na mbili nukta mbili. Kati ya hizo kiasi cha Dola milioni saba zinalipwa kwa Serikali ya Tanzania, Dola za milioni sita zikiwa ni fidia na Dola milioni moja ikiwa ni riba.
Mheshimiwa Spika, Serikali imefuatilia taarifa ya hasara kwa Serikali ya Tanzania ya Dola za Kimarekani milioni themanini iliyotajwa na Mheshimiwa Zitto Mbunge wa Kigoma Mjini na hatukupata usahihi wake. Hata hivyo, taarifa ya hasara ya dola milioni themanini imetajwa katika taarifa yenye kichwa cha habari How Tanzania was Short Changed in Stanbic Bribery Payback iliyochapishwa katika gazeti la The Guardian la tarehe 16 Disemba, 2015, likinukuu taarifa ya Corruption Watch ya Uingereza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa taarifa haikutoa maelezo ya namna hasara ya dola milioni themanini ilivyopatikana na kwa kuwa, taarifa iliyonukuliwa kutoka corruption watch pia haielezi jinsi hasara hiyo ilivyokokotolewa, Serikali inashauri Mheshimiwa Mbunge awasilishe taarifa alizonazo tuone iwapo ina vigezo vya kutosha kuisaidia Serikali kujenga hoja ya madai ya hasara hiyo.
Mheshimiwa Spika, pamoja na maelezo hayo napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Benki Kuu imeiandikia Benki ya Stanbic barua ya kusudio la kuitoza faini ya shilingi bilioni tatu kwa kosa la kufanya miamala inayokiuka sheria na kanuni za benki na taasisi za fedha. Aidha, sheria inaitaka Benki ya Stanbic kutoa utetezi katika kipindi cha siku 20 ambacho kimekwisha tarehe 30 Januari. Kwamba Stanbic imewasilisha taarifa ya utetezi wao Benki Kuu na utetezi wao unafanyiwa kazi kwa sasa. Endapo Benki Kuu haitaridhika na utetezi huo Benki ya Stanbic italazimika kulipa faini hiyo.