Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Primary Question

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: - Je, upi mkakati wa kuwapa Wananchi ardhi mbadala wanapoondolewa kwenye maeneo yao kupisha uhifadhi na miradi ya mkakati?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa tena nafasi niulize swali la nyongeza, kwanza nitoe shukurani nyingi kwa majibu mazuri ya Serikali kupitia kwa Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Jerry Silaa ambaye alikuwa Mwenyekiti wangu Kamati ya PIC, nimpongeze kwa kuwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu majibu yake yapo sawasawa lakini watendaji wakati wa kutekeleza huwa hawaweki bayana sheria inasemaje badala yake wanakuja wanakuambia jamani hili eneo linachukuliwa kwa ajili yakazi hii na hii ya Serikali ninyi mnatakiwa muondoke, mtapata fidia kwa maendelezo ambayo mlikuwa mmefanya.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muhimu wakati wa kuhamisha wananchi kwenye maeneo yao watoe maelekezo kwamba watapata nini na nini kulingana na eneo ambalo linachukuliwa either kwa uhifadhi au utekelezaji wa miradi?

Pili, swali langu ni je, Waziri utakuwa tayari kuambatana na mimi tuende tukafanye mkutano uwaeleze wananchi maeneo ya Momela pamoja na KIA ambao wanatakiwa wahame?

Name

Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Answer

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa majibu kwa maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa John Danielson Pallangyo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, naomba kutumia Bunge lako tukufu kuagiza Wathamini wote na Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali kuhakikisha inatoa elimu stahiki kwa wananchi pindi ambapo maeneo yao yanatwaliwa kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maendeleo. Wananchi waelezwe wazi takwa la sheria kwa wale wanaotaka kuchukua fedha taslimu kwa niaba ya ardhi yao na kwa wale ambao wanataka kutafutiwa ardhi mbadala.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, pamoja na kwamba niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Dkt. John Pallangyo lakini eneo la KIA na eneo la Momela ni maeneo ambayo yanaangukia kwenye vile vijiji 975 ambapo wananchi walikuwa wameingia kwenye maeneo ya hifadhi na wengine wameingia kwenye eneo la Uwanja wa Ndege wa KIA. Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan iliona ni busara kuwafidia kwa yale maendelezo waliyoyafanya, maeneo haya fidia yao wanayolipwa haihusishi ardhi ambayo wamekuwa wakiikalia. Baada ya Bunge hili Mheshimiwa Dkt. Palangyo tutaongozana pamoja kwenda kutoa elimu kwa wananchi wa Jimbo lako, ahsante. (Makofi)