Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mrisho Mashaka Gambo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arusha Mjini

Primary Question

MHE. MRISHO M. GAMBO aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya mapitio ya malipo ya mkupuo (kikokotoo) ya asilimia 33 kwa wafanyakazi?

Supplementary Question 1

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kanuni mpya ya mafao kwa wafanyakazi imekwenda kupunguza asilimia 50 ya malipo ya mkupuo ya wastaafu. Pia imepunguza miaka inayokadiriwa mtumishi kuishi baada ya kustaafu kutoka miaka kumi na tano na nusu mpaka miaka kumi na mbili na nusu.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kurejesha Kanuni ya mwaka 2017 ambayo ilikuwa imeweka maslahi mapana zaidi kwa wastaafu?

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwenye majibu ya Serikali imesema kwamba mifuko itafanya tathimini ifikapo mwezi Juni mwaka huu 2023, mpaka tunavyozungumza tayari imeshapita miezi mitano.

Je, tunaweza tukapata majibu ya tathimini hiyo ya Serikali kupitia Bunge lako Tukufu?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Gambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni katika mifuko hii. Wote tunatambua tulikuwa na mifuko mingi hapo awali, mifuko ya PPF, LAPF, PSSSF na mifuko mingine mingi tu. Uendeshaji wake ulikuwa wa gharama kubwa sana kwa sababu ya menejimenti lakini ilitengenezwa katika misingi ya kuwa na ushindani. Ikawa ni wazo na mfumo wa Serikali wa kuweza kuboresha zaidi na kuangalia maslahi kwa sababu ya uhalisia na sera za wakati huo na mabadiliko ya hali ya kiuchumi ikaona ifanye actuarial evaluation ambayo ilileta majibu kwa wakati huo kwamba ilifaa kuweza kuangalia walio wengi zaidi na kuweza kuwapa manufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, asilimia 81 ya hali ya kikokotoo cha sasa inawapa manufaa ya kuwa na mkupuo mkubwa. Asilimia 19 wanabaki kuwa na mkupuo ambao ni wa wastani lakini mapato ya kila mwezi yameongezeka. Kwa hiyo, tathimini baada ya miaka mitatu ambayo tumeifikia sasa na nikijibu hoja yake ya swali la pili kwamba tunaendelea na tathimini na sasa tumpe majibu ya tathimin.

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini ni tafiti sasa huwezi ukataka kwa wakati wowote kuweza kupata majibu yake ni mpaka pale ambapo itakamilika. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ina nia njema sana kukitoa kikokotoo hiki asilimia 25 mpaka 33. Si ajabu tathimin hii itakapotoa majibu tukiangalia ustahimilivu wa mfuko na maslahi ya wafanyakazi wetu ambao ni vipenzi vya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan tutaenda kutoa faida kubwa kwa upande wao na kuweza kuwasaidia Watanzania ambao wametumikia Taifa.