Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:- Waandishi wa Habari wanafanya kazi nzuri katika kuelimisha jamii. Je, ni lini Serikali itaanzisha mfumo utakaotambua kazi zinazofanywa na tasnia ya habari?

Supplementary Question 1

MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Sheria ya Huduma za Habari ya mwaka 2016 inaitaja kazi ya uandishi wa habari kuwa ni jukumu la kisheria. Serikali inawachukulia hatua gani watu wanaowazuia waandishi wa habari kutekeleza majukumu yao? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hivi karibuni kumekuwa na matukio kadhaa ya waandishi wa habari kuzuiwa kufanya kazi zao kama vile RC kuvamia kituo cha Clouds, baadhi ya waandishi kuvamiwa wakiwa kwenye mkutano wa CUF, baadhi ya Wakuu wa Wilaya kuwakamata waandishi wa habari na kuwaweka ndani na hata jana kule Arusha katika Shule ya Msingi ya Lucky Vincent waandishi wa habari kumi walikamatwa wakiwa wanatimiza majukumu yao. Ni lini Serikali itaacha tabia hii mbaya ya kuwakamata kamata waandishi wa habari wakiwa kwenye majukumu yao? (Makofi)

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana kwa maswali yake na kwa kutambua kwamba Sheria ya Vyombo vya Habari ya mwaka 2016 inahimiza kwamba kazi ya waandishi wa habari ni jukumu la kisheria, nadhani sote tunakubaliana na hilo. Hata hivyo, anaposema kwamba kuna watu wanaozuiwa kufanya kazi zao, mimi naamini kwamba kama kweli waandishi wa habari wanafuata maadili na wanatafuta habari kwa ajili ya kujenga na siyo kuvuruga nchi, siamini kabisa kwamba kuna watu wanaoweza kuwazuia.
Sera yetu ya Habari na Utangazaji ya mwaka 2003 inahimiza kwamba taasisi zote za Serikali na wadau wote wa habari kutoa taarifa kwa wanahabari na inahimiza kabisa kwamba wale Maafisa Habari katika Mikoa na Halmashauri wawe tayari kutoa ushirikiano kwa wanahabari ili kusudi wanahabari waweze kutekeleza majukumu yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama kuna hili la watu wanaozuia, mimi naomba baadaye tuonane na Mheshimiwa Devotha Minja aweze kuniambia ni wapi kwa sababu ndiyo kwanza nasikia hilo. Sera yetu inahimiza kwamba ni wajibu kwa Maafisa wa Habari kuwapa ushirikiano wanahabari kwa sababu jukumu lao linatambulika kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili Mheshimiwa Waziri alilitolea ufafanuzi vizuri sana wakati anahitimisha hotuba yake hapa Bungeni. Kwa hiyo, naomba nisirudie tena maneno ambayo aliyasema Mheshimiwa Waziri hapa Bungeni.