Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:- Mchango wa kazi za wasanii umeonekana katika kutoa ajira lakini bado wasanii wanakabiliwa na changamoto mbalimbali za kuhujumiwa kazi zao ambapo Mheshimiwa Rais ametoa maagizo mbalimbali ya kushughulikia watu wanaohujumu kazi za wasanii. Je, mpaka sasa ni hatua gani zimechukuliwa?

Supplementary Question 1

MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyoeleza Naibu Waziri, kazi za wasanii ni kuburudisha, kuelimisha, kuonya na kukosoa, wasanii wamekuwa wakifanya kazi hizi hata wakati wa kampeni tulishuhudia wasanii walivyofanya kazi yao vizuri na wakati mwingine waliimba nyimbo za kuponda upinzani na mlikuwa mkishangilia. Jambo la kushangaza hivi sasa wasanii wakiimba nyimbo za kukosoa Serikali wanashughulikiwa na mfano mzuri ni Ney wa Mitego pamoja na Roma Mkatoliki.
• Swali la kwanza, je, ni wakati gani sasa kazi hizi za wasanii zinathaminika?
• Swali la pili, kwa bahati mbaya sana Rais ametoa maagizo ya wale ambao wamehujumu kazi za wasanii na kuacha kabisa kuwawajibisha Serikali yake ambayo imeshindwa kabisa kuthamini kazi nzuri iliyofanywa na Marehemu Mzee Francis Ngosha ambaye amekufa akiwa maskini wa kutupwa.
Je, Serikali inataka kukamata kazi za wasanii wakati ninyi wenyewe mmemuhujumu Mzee Francis Ngosha ambaye mpaka sasa hivi hana lolote, amekufa na hakuacha alama yoyote katika familia yake? (Makofi)

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli maswali yake yako nje kidogo na swali la msingi, lakini kwa sababu tu ya kumbukumbu tulizonazo, swali lake la kwanza linalouliza kwamba ni wakati gani kazi za wasanii zinathaminiwa? Kama alivyosema mwenyewe, kwamba kazi ya sanaa ni kuburudisha, kuelimisha, kuonya, kukosoa na kadhalika, niseme tu kwamba kazi za wasanii tunazithamini wakati wote hasa wakati zinapoelimisha, zinapoburudisha na kufanya kazi zile ambazo zinalijenga Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kusema kwamba wasanii huwa wanashughulikiwa wakiikosoa Serikali, nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hizi za sanaa zinasimamiwa na sheria. Tunayo Sheria ya BASATA Namba 23 ya mwaka 1984, tuna Sheria nyingine Namba 4 ya Bodi ya Filamu ya mwaka 1976 na tuna Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki Namba 7 ya mwaka 1999. Kwa hiyo, tunachohitaji ili tuweze kuzithamini kazi hizi ni kwamba wasanii wazingatie sheria, wafuate sheria na taratibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa wasanii ambao tunaona kwamba wameenda kinyume, hatua huwa zinachukuliwa na hatua zenyewe, kwa mfano kuna msanii mmoja anaitwa Nikki Mbishi ambaye alipewa tu onyo kutokana na kuweka picha ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne katika wimbo wake I am sorry JK. Hizo ni hatua tu ambazo huwa tunazichukua ili wasanii hawa wafuate sheria. Sheria ya BASATA inahitaji wasanii hawa wapitishe nyimbo zao BASATA ili ziweze kukaguliwa kabla hazijatolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakiwa wamepitia kule ina maana kwamba watatoa kitu ambacho kinazingatia sheria na kinafuata maadili, sasa huu ni ukiukwaji wa maadili.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwingine ambaye ameshawahi kupewa onyo ni Diamond kupitia kwa Meneja wake, ambaye alitumia majina ya viongozi bila kufuata utaratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Ney wa Mitego, huyu aliimba wimbo wake wa Wapo ambapo ulifungiwa na BASATA kwa muda, lakini baadaye ulifunguliwa baada ya kuwa na makubaliano ya jinsi ya kuuboresha huo wimbo. Huyo mwingine Roma, hakuna hatua ambayo imechukuliwa na Serikali kwa mwaka huu kuhusu msanii huyo na ninadhani ninyi ni mashahidi kwamba alijieleza yeye mwenyewe kwa vyombo vya habari na Mheshimiwa Waziri pia alikuwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ambalo linamhusu Marehemu Francis Ngosha na Mheshimiwa Devotha anadai kwamba Serikali imemhujumu, hii siyo kweli, hakuna hujuma. Kimsingi yapo majina mezani mpaka sasa kama matatu hivi yanayohusiana na ubunifu wa nembo tunayoitumia, ambayo ni nembo ya Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mpaka sasa bado haijajulikana ni nani hasa ambaye ni mbunifu wa nembo hii. Kwa sababu kwa mfano, yupo Marehemu ambaye alishatangulia mbele za haki muda mrefu anayeitwa Abdallah Farhan wa Zanzibar, yeye vielelezo tayari vimeshakutwa katika kumbukumbu zake jinsi alivyokuwa akibuni nembo yetu ya Taifa, nembo ya Kenya pamoja na nembo ya OAU kipindi hicho alipokuwa akisoma Makerere University. Kwa hiyo, yapo majina ambayo yanadaiwa kwamba yalishiriki katika kutengeneza nembo hii. Ninaomba sana… (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wataalam wafanye kazi ya kutambua ni nani hasa ambaye alishiriki kubuni. Kwa sababu Marehemu Francis yeye anajulikana kama ni mchoraji, lakini siyo mbunifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme tu kwamba labda swali la Mheshimiwa Devotha Minja ni ishara ya wazi kwamba kuna uhitaji mkubwa sana wa kuwa na orodha ya wasanii na kazi ambazo wamezifanya na ni kitu ambacho sasa hivi Wizara tumeanza kukifanya ili kusudi tuwe na orodha ya wasanii wote katika nchi yetu na kazi ambazo wanazifanya ili mwisho wa siku utata kama huu usiweze kutokea tena. (Makofi)

Name

Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:- Mchango wa kazi za wasanii umeonekana katika kutoa ajira lakini bado wasanii wanakabiliwa na changamoto mbalimbali za kuhujumiwa kazi zao ambapo Mheshimiwa Rais ametoa maagizo mbalimbali ya kushughulikia watu wanaohujumu kazi za wasanii. Je, mpaka sasa ni hatua gani zimechukuliwa?

Supplementary Question 2

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.
Moja kati ya changamoto kubwa za wasanii wa Tanzania ni kuibiwa kazi zao, lakini pia kutonufaika na kazi zao kwa sababu ya kazi hizo kutolindwa ipasavyo. Tunaona kuna upungufu mkubwa sana kwenye Sheria Namba 7 ya mwaka 1999, Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki.
Je, Serikali haioni kwamba huu sasa ni muda muafaka wa kuileta sheria hii kwenye Bunge lako Tukufu tuweze kuibadilisha na kuirekebisha ili iweze kusaidia wasanii wa Tanzania waweze kupata haki zao, kwa sababu wengi wanakufa masikini, wanaibiwa kazi zao mtaani lakini wanaowaibia tunawajua?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hili suala tayari COSOTA imeshaliona, hii ni Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki. Kwa kuanzia imeanza kufanya utaratibu wa kubadilisha kifungu namba 46. Kwa hiyo, mchakato huu unaendelea, tuwe na subira ili marekebisho yaweze kufanyika ikiwa ni pamoja na kanuni zake. Ahsante.