Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:- TEHAMA imekuwa kichocheo cha maendeleo na hivyo kurahisisha ulipaji wa gharama (bills) mbalimbali kupitia miamala kwa njia ya simu. Mathalani, muda wa maongezi, ving’amuzi, umeme, kodi na laini mbalimbali. Je, mlipaji aweke ushahidi wa aina gani katika kumbukumbu ngumu (hard paper) ili wakaguzi wa TRA waone au TRA itaridhika kwa kumbukumbu ya muamala?

Supplementary Question 1

MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kanzidata zinatunzwa na hizi kampuni za simu na sio sisi wamiliki wa hizi kampuni na kwa kuwa inaweza ikatokea simu ikapotea au ikaibwa na kumbukumbu mtu asiwe nayo. Sasa je, Serikali iko tayari kupokea maelezo ambayo yatakuwa yameandikwa kwenye vocha ya malipo ambapo mfanyabiashara ameweka tu ile reference number, je Serikali itakuwa tayari kuikubali?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, tulivyoanzisha mifumo ya electronic devices (electronic signature device, electronic fiscal device na electronic tax register) wafanyabiashara wakubwa (large tax payers) walipewa bure kwa maana ya kwamba waliweza ku-claim kutoka kwenye uandaaji wa VAT return. Sasa kwa mpango huo ambao ulifanyika kwa wafanyabiashara wakubwa, je, Serikali haioni haja sasa ikatoa hizi EFD bure kwa wafanyabiashara wadogo au ikaweka ruzuku ambapo itawawezesha…

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwenye majibu yangu ya msingi nimesema kifungu cha 35(3) kinamtaka mlipa kodi mwenyewe kutunza kumbukumbu zake kwa miaka mitano mfululizo. Kifungu hiki kinaweka utaratibu wa kwamba unapokuja kukaguliwa na watu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania wanakutaka uwe na hizi kumbukumbu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe tu walipa kodi wetu wajitahidi kuwa na hizi kumbukumbu kama sheria inavyotuelekeza lakini kwa jitihada za Serikali yetu ya Awamu ya Tano makampuni yote ya simu yametakiwa kupitisha miamala yao katika kanzidata yetu pale Kinondoni. Kwa hiyo, kama mlipa kodi atakuwa amepoteza kumbukumbu zake ni rahisi zaidi kuzipata taarifa zake pale katika kituo chetu cha Kinondoni.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, napenda kulihakikisha Bunge lako tukufu kwamba ni sahihi tuligawa mashine hizi kwa wafanyabiashara hasa kwa Mkoa wa Dar es Salaam na sasa tunaandaa utaratibu wa kuwafikia wafanyabishara wetu wote, lakini sio kwa kuwapa bure kwa sababu hata wale wa mwanzo hawakupewa bure, kilichofanyika anapewa mashine ya EFD halafu anakatwa kwenye kodi yake ambayo alitakiwa kuilipa Serikalini.
Mheshimiwa Spika, tunaendelea na mfumo huo na kuanzia tarehe 1 Julai, Mamlaka ya Mapato Tanzania itaanza yenyewe kugawa mashine hizi badala ya kutumia mawakala ambao wametuingiza gharama zisizo za msingi kwa wafanyabiashara wetu na tuna uhakika tunapolichukua jambo hili hata gharama za mashine hizi zitakuwa ndogo kwa wafanyabiashara wetu.