Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rose Cyprian Tweve

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:- Serikali imeweka utaratibu wa kuzitaka Halmashauri zote za Wilaya kutenga asilimia tano ya mapato ili kuwawezesha wanawake na vijana kupata mikopo:- Je, ni akinamama wangapi au vikundi vya wanawake vingapi vimenufaika na mikopo hiyo katika Halmashauri za Wilaya ya Mufindi, Kilolo, Iringa Mjini na Iringa Vijijini?

Supplementary Question 1

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu yako Mheshimiwa Waziri, kwangu naona hayajitoshelezi. Nilitegemea ungenipa ni kiasi gani pesa zilitolewa kwenye hivi vikundi vya akinamama kila Wilaya.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kumekuwa na urasimu mkubwa sana wa utoaji wa hizi pesa kwa akinamama especially kwa Wilaya zangu za Mufindi, Iringa Mjini, Kilolo na Iringa Vijijini: je, huoni umuhimu wa kutoa tamko rasmi kwa Wakurugenzi ambao watakwenda kinyume na utaratibu wa utoaji wa pesa hizi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, je, huoni wakati sasa umefika kwa Wabunge wa Viti Maalum kusimamia zoezi zima la utoaji wa pesa hizi kwenye vikundi vya akinamama? After all, wao ndio wametuchagua sisi kuwa wawakilishi wao. Ahsante sana.

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumpongeza dada yangu Mheshimiwa Rose Tweve kwa ajenda yake na swali lake. Ni kweli, katika analysis, maana yake nilizungumza jinsi gani wanawake na vijana wamefikiwa. Nilichambua mchanganuo mbalimbali katika kila Halmashauri. Kwa figure halisi ni kwamba wanawake walipata sh. 339,487,000/= wakati vijana walipatana shilingi milioni 98. Hapa kuna mchanganuo mdogo wa kila Halmashauri kuona ni jinsi gani ilishiriki katika vile vikundi ambavyo i nimevibainisha awali kwamba vilipewa zile fedha.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika Mkoa wa Iringa ni kwamba, kila Halmashauri, kama nilivyosema, kwa figure, akinamama walipata karibu shilingi milioni 339 na vijana milioni 98. Kwa suala zima la kutoa maagizo kwa Wakurugenzi, hili lilikuwa ni jambo langu la msingi zaidi. Nilizungumza siku tulipohitimisha bajeti yetu hapa, tukasema kwa sababu mwaka huu karibu takriban shilingi bilioni 56 zitakwenda kwenye vikundi vya akinamama na vijana, katika ule mgao wa asilimia tano tano. Nilisema katika bajeti yetu kwamba Wakurugenzi wote wa Halmashauri wana kila sababu kuhakikisha wanatekeleza hili.
Pia niliainisha tena, nikasema kwa sababu pesa za ndani maamuzi yake yanafanyika ndani ya Halmashauri, baada ya kupokea kwamba ni kiasi gani kimekusanywa, Kamati ya Fedha sasa inaweza kuhakikisha kwamba katika mwezi ule ule inatoa ule mgawanyo wa asilimia tano kwa tano kwa vijana na kwa akinamama.
Kwa hiyo, niliwahimiza Wabunge wote, kwa sababu sisi ni Wajumbe katika hizo Halmashauri zetu, tuhakikishe tunapokusanya own source tuwe wa kwanza kuhakikisha kwamba tunazielekeza pale pale, kwa sababu pesa hizi haziendi Hazina wala haziendi TAMISEMI, zinaishia katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa Wakurugenzi wetu kwamba waende wakalisimamie hili. Vile vile niseme tena, Madiwani wote wanaingia katika Kamati ya Fedha na yale Mabaraza yetu ya Madiwani wahakikishe fedha hizi tano kwa tano zinakwenda kwa mujibu wa taratibu tulizojiwekea.
Mheshimiwa Spika, kuhusu Wabunge Wanawake kusimamia jambo hili kwa karibu; naomba niwaambie, hili ni jukumu letu sisi sote. Akinamama, vijana na Wabunge wote humu tuna jukumu hilo. Mimi lengo langu ni nini? Ni kwamba kila Mbunge ataona kwamba jambo hili ni la kwake. Mama akinufaika katika Jimbo hilo, maana yake unakuza uchumi wa watu katika eneo hilo.
Mheshimiwa Spika, hali kadhalika, vijana wakinufaika, maana yake unakuza uchumi wa vijana katika eneo hilo. Kwa hiyo, ni jukumu letu sisi sote, twende sasa tukalisimamie hili kwa nguvu kubwa kwa ajili ya mustakabali wa uchumi wa nchi yetu.