Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:- Mheshimiwa Rais alitoa tamko kuwa Wazauni wote wanaoidai Serikali walipwe:- Je, tokea tamko hilo litolewe ni Wazabuni wangapi wameshalipwa?

Supplementary Question 1

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali madogo tu mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, naomba niipongeze Serikali kwa majibu yake mazuri, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa tamko lake ambalo limehakikisha kwamba wazabuni wote wanalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna baadhi ya wazabuni wakiwemo hata wa Mkoa wangu wa Iringa wameshafanyiwa uhakiki zaidi ya mara moja, lakini wanadaiwa na mabenki, wanadaiwa na TRA na wanatishiwa mpaka kuuziwa mali zao:-

Je, Serikali inawasaidiaje wasifilisiwe? Maana wengi wao tayari wameshapata maradhi na kufa na wengine wameshafilisika kabisa kwa ajili ya madeni ambayo wanaidai Serikali.

Swali langu la pili; je, ni vigezo gani sasa vinatumika kwenye malipo ya madeni ya wazabuni hao?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la kwanza kuhusu msaada wa Serikali ili wananchi wetu wasifilisiwe, naomba kumwambia Mheshimiwa Rita na kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali yetu kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tunalipa madai pale yanapokuwa yamehakikiwa. Wananchi wetu hawa wa Mkoa wa Iringa, kama wapo ambao madeni yao yamehakikiwa na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Ndani wa Serikali, basi tumekuwa tukiwasaidia mmoja baada ya mwingine wanapofika na kuwasilisha nyaraka zao kuonyesha kwamba wamehakikiwa na sisi kujiridhisha kwamba wapo kwenye orodha ya kulipwa ndani ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Ritta na nimpongeze kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akiifanya katika kuwatetea wananchi wa Iringa. Ameshakuja siyo mara moja wala mara mbili ofisini kwangu, naomba tuendelee kushirikiana ili tuwasaidie wananchi wetu ili wasifilisiwe na ili wasiendelee kupata maradhi kama wapo kweli waliopata maradhi. Tuendelee kushirikiana tuwasaidie wananchi hawa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, ameuliza ni vigezo gani vinavyotumika kulipa madai haya ya wazabuni pamoja na wakandarasi wengine? Kwanza kabisa ni kuhakikisha deni limehakikiwa na limekidhi vigezo vya kuwa deni halali. Hicho ni kigezo cha kwanza kwamba deni hilo linalipwa.

Mheshimiwa Spika, sababu ya pili au kigezo cha pili ambacho kinapelekea kulipwa, tunaangalia deni lile kama hali-attract riba kwa Serikali, lakini pia kwa yule ambaye anaidai Serikali. Kama deni hili lina-attract riba tunayapa kipaumbele ili Serikali isiendelee kuumia na ili tusiendelee kuwaumiza wananchi wetu ambao wanaidai Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, kigezo cha tatu ni kuhakikisha kwamba ukubwa wa deni lenyewe, kwa wale ambao wana madeni ambayo siyo makubwa na ambao ndio wengi tumekuwa tukiwapa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunawalipa madeni yao kwanza ili kuweza kuchachua uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mwaka 2017/2018 Bunge lako Tukufu lilitupitishia bajeti ya shilingi trilioni moja kwa ajili ya kulipa madeni haya na Serikali ililipa zaidi ya shilingi trilioni 1.096 kwa sababu dhamira ya Serikali yetu ni njema kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kigezo cha nne, ni umri wa deni. Madeni yale ambayo yamekaa kwa muda mrefu na tayari yamehakikiwa, tumekuwa tukiyapa kipaumbele na kuhakikisha yote yanalipwa ili kuwawezesha wananchi wetu kuendelea kushiriki katika shughuli za kiuchumi.