Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Flatei Gregory Massay

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Vijijini

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:- Madiwani nchini wanafanya kazi kubwa sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea posho na mishahara au maslahi yao?

Supplementary Question 1

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa Halmashauri hazina uwezo wa kuwalipa Madiwani na mpaka sasa Madiwani wengi wamekopa posho zao; na kwa kuwa mapato madogo na hali hii inapelekea Madiwani kutolipwa stahiki zao: Je, Serikali ina mpango gani kubadilisha namna hii ili Serikali ilipe toka Hazina kama walivyo Watumishi wengine sasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wenyeviti wa Vitongoji na Wenyeviti wa Vijiji nao wanafanya kazi sawasawa na Madiwani na Watendaji, hao Ma-VEOs na WEOs wanalipwa mishahara: Je ni lini sasa Serikali itawaona Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji ili kuwalipa posho au mshahara?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru. Swali lake la kwanza anapendekeza kwamba Waheshimiwa Madiwani walipwe posho kutokea Hazina na kwa maelezo yake anasema kwamba kuna Halmashauri ambazo hazina uwezo. Ukweli ni kwamba Halmashauri ambayo haina uwezo wa kujiendesha inapaswa kufutwa kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, lazima vyanzo viwe vimeainishwa na vinasimamiwa na hii hatujapata malalamiko rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoelezea ni kwamba Halmashauri kwa mapato yake ya ndani wanajipangia namna ya kuweza kulipa Waheshimiwa Madiwani. Kama Serikali itapata uwezo mkubwa zaidi ya huu uliopo sasa, hili jambo litafanyiwa kazi. Kwa sasa Halmashauri zote zinapaswa kulipa na tunajua kuna Halmashauri ambazo Waheshimiwa Madiwani wanazidai fedha mpaka sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshaelekeza kila Mkurugenzi ahakikishe kwamba Madiwani wanalipwa stahiki zao kwa sababu wanafanya kazi kubwa. Swali lake la pili, anapendekeza pia kwamba kuwe na mpango wa kulipa Wenyeviti wa Mitaa. Ni kweli, nami ni Mwenyekiti wa Mtaa Mstaafu kule Kivule Dar es Salaam Ukonga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maelekezo ya Serikali kwamba kila makusanyo yote ya Halmashauri asilimia 20 inabidi irudi katika Mitaa yetu na Vijiji, inawezekana jambo hili halitekelezwi vizuri. Naomba niwaelekeze Wakurugenzi, Wenyeviti wa Vijiji kwa sasa, ile asilimia ambayo inapaswa kurejeshwa baada ya kodi kukusanywa katika eneo lao, ipelekwe na waweze kulipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuendelea kuwalipa asilimia nyingine zaidi hii au Serikali Kuu ichukue jukumu hili, kwa kweli itategemea uwezo wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Name

Rev. Peter Simon Msigwa

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Iringa Mjini

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:- Madiwani nchini wanafanya kazi kubwa sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea posho na mishahara au maslahi yao?

Supplementary Question 2

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri, asilimia 20 ambayo inatengwa ili irudi kwa ajili ya Wenyeviti wa Mitaa, kuna Halmashauri nyingine hiyo asilimia 20 ni ndogo sana. Ni kwa nini Serikali isitoe commitment ili hawa Wenyeviti wa Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji wapate mshahara kwa sababu wao ndio wanafanya kazi kubwa sana katika shughuli zote za maendeleo huko tunakotoka?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nia njema ya Serikali tungeweza kuwalipa Wenyeviti wa Mitaa mishahara. Hapa tunazungumzia hali ya uwezo wa Serikali kufanya kazi. Wenyeviti wa Mitaa ni wengi sana, pamoja na kazi kubwa wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoelekeza, pamoja na kwamba hayo mapato ni madogo, kwa kinachopatikana, kuna Wenyeviti wa Mitaa hawalipwi kabisa fedha hizi na tuna malalamiko mengi wameleta. Tumeelekeza Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakurugenzi, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wahakikishe hawa watu wanalipwa stahiki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kuweza kuwalipa kwa sasa, tumelichukua, tutalifanyia kazi. Uwezo wa Serikali ukiruhusu, hawa viongozi wenzetu watalipwa stahiki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:- Madiwani nchini wanafanya kazi kubwa sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea posho na mishahara au maslahi yao?

Supplementary Question 3

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini ukweli ni kwamba pamoja na maelekezo yanayoelekezwa kule chini, viongozi hawa wa Mitaa na Vijiji, Vitongoji hawalipwi posho zao; na kwa kuwa Serikali kwa namba ya viongozi hawa kuwa kubwa inashindwa kuongeza posho zao:-

Serikali haioni umefika wakati sasa kufikiria uwezekano wa kuwalipa kiwango fulani cha pesa viongozi hawa pale wanapomaliza muda wao wa Uongozi?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona Waheshimiwa Wabunge wanazungumzia posho za Madiwani na posho za Wenyeviti wa Mitaa; naomba nitumie nafasi hii kusema tu kwamba wakati tunamalizia hoja yetu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, suala la posho za Madiwani zile ambazo zilikuwa zimezungumzwa, Mheshimiwa Waziri ameshatoa maelekezo kwa Madiwani wote wa Halmashauri watapata Waraka wa maelekezo kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuondoa sintofahamu ya posho za Madiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali alilouliza Mheshimiwa Mkundi, tulipokee; ni kweli kwamba Wenyeviti wa Mitaa baada ya kustaafu kuna kiwango cha fedha wanapaswa kulipwa. Sasa maoni ya Mbunge ni kwamba tuangalie namna ya kuongeza kiwango hiki (lump sum amount) kama watasema ni shilingi 500,000/= au shilingi 1,000,000/= kwa mkupuo itaweza kuwasaidia. Jambo hili tunalipokea, tunalifanyika kazi, kadri uwezo wa Serikali utakavyoruhusu, tutalitekeleza kwa sababu ni jambo jema kwa ajili ya viongozi wenzetu hawa.

Name

Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:- Madiwani nchini wanafanya kazi kubwa sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaongezea posho na mishahara au maslahi yao?

Supplementary Question 4

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa jambo muhimu kama hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaofanya bidii na kushirikiana na Wabunge ni Madiwani na Wenyeviti katika kuhamasisha maendeleo katika maeneo yao; sasa kama Halmashauri inaweza kuwa na uwezo wa kulipa posho zaidi: Je, Serikali inaweza ikaruhusu Halmashauri ile yenye uwezo kuongeza posho kwa hawa ambao ndio wanaoweza kuongeza mapato hayo?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge sawa na Wabunge wengine wote ambao wameendelea kuwasemea Waheshimiwa Wenyeviti wa Mitaa na Waheshimiwa Madiwani, nao ni viongozi wenzetu na hakuna namna ya kuweza kuwapuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza hapa kwamba wakati wa Bajeti kulikuwa na mjadala; na kweli kuna Waraka ambao umepelekwa katika Halmashauri zetu ambao unaelekeza fixed amount kulipwa kwenye posho za Madiwani ukiacha ile posho ya mwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema Mheshimiwa Waziri aliahidi mbele ya Bunge lako Tukufu na naomba niseme, bado ametoa ametoa maelekezo, ndani ya muda siyo mrefu sana, Waraka kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia Katibu Mkuu utaenda kwenye Halmashauri zote na suala hili la kulipana Madiwani kulingana na uwezo wa Halmashauri litatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.