Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Maryam Salum Msabaha

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:- Kumekuwa na baadhi ya Askari wa barabarani wanaosimamisha magari hasa yale ya safari ndefu wakitokea vichakani (kujificha) na hatimaye wakati mwingine kusababisha ajali:- Je, ni Askari wangapi kama hawa wameshachukuliwa hatua za kinidhamu?

Supplementary Question 1

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, askari wa usalama barabarani wamekuwa na matukio ya kujificha vichochoroni, wanajificha vichakani sasa magari yanakuwa yanakwenda kwa speed na wanasimamisha gari kwa ghafla na huku nyuma kuna msururu wa magari. Hili Morogoro imeshawahi kutokea na Tukuyu imeshawahi kutokea kutokana na Askari wa Usalama Barabarani.

Je, Serikali ina mikakati gani kuwapitia askari wote ambao wanakaa kwenye vituo vya Usalama Barabarani kuhakiki hii tabia ya kujifichaficha vichochoroni kwani hakuna mbinu mbadala ya kusimamisha magari mpaka mtu utoke vuup na kusimaisha gari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa matrafiki wa barabarani uweledi wao wakufanya kazi baadhi yao ni changamoto hasa kwa barabarani. Je, Serikali ina mikakati gani kuwapeleke matrafiki wote kuwapa mafunzo ya mbinu mbadala na zile tochi kuzitumia kwa sababu zile tochi wananchi wamekuwa wakizilalamikia sana, wanaweza kusema unapigwa tochi wanasema inakwenda speed, lakini ile speed haifanani na ile tochi? Naomba majibu ya Serikali.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili kwa pamoja ya Mheshimiwa Maryam Msabaha kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu swali langu la msingi kwamba tumefanikiwa kupunguza ajali kwa asilimia 43 na hususan ambazo zinasababishwa na magari ya abiria, mafanikio hayo pamoja na mambo mengine yalisababishwa kutokana na mbinu na uweledi wa askari wetu katika kubaini mbinu na njama ambazo zinatumika na madereva wasiokuwa waaminifu kuweza kukiuka sharia. Kwa hiyo hili suala ambalo amelizungumza kwa askari kukaa barabarani kuweza kujificha na mengine yote, malengo yalikuwa ni ya nia njema, lakini kama kutakuwa na upungufu katika utekelezaji wa hayo kwa baadhi ya askari basi tunachukua kama ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge afahamu kwamba dhamira ya Jeshi letu la Polisi kupitia Vikosi vya Usalama Barabarani si kuburuza wananchi, lakini kusaidia wananchi kuokoa maisha yao hususan kwa wale madereva ambao hawafuati sheria.

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:- Kumekuwa na baadhi ya Askari wa barabarani wanaosimamisha magari hasa yale ya safari ndefu wakitokea vichakani (kujificha) na hatimaye wakati mwingine kusababisha ajali:- Je, ni Askari wangapi kama hawa wameshachukuliwa hatua za kinidhamu?

Supplementary Question 2

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kumekuwa na tatizo kubwa wananchi kubambikizwa kesi hasa kwenye hizi kamera, mtu unapigwa kamera ukienda kuhoji wanasema kwamba imekosewa namba ya gari kwa hiyo wananchi wengi wamekuwa wanabambikiziwa makosa ambayo si ya kwao. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na kamera ambazo zimekuwa zinawabambikia wananchi makosa ambayo siyo ya kwao.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi haya ya teknolojia tumeanzia na kamera, tuna mfumo VTS na tuna mambo mengine mengi ambayo tunaelekea nayo huko, yote haya yana dhamira ya kupunguza hizo dhana dhidi ya askari wetu kuhusiana na kubambikia watu makosa.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba matumizi ya tochi yamekuwa yakitusaidia sana. Hata hivyo, ikiwa kuna changamoto upungufu wa kimaadili wa baadhi ya askari wetu na hilo hatuwezi kulikataa kwa sababu askari nao ni binadamu huwezi kuwa na askari wote hawa wakose wawili watatu ambao watakuwa na upungufu wa kimaadili, tumekuwa tukiendelea kuchukua hatua pale ambapo tunapata taarifa na uthibitisho juu ya kubambikia wananchi makosa ambao hawahusiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumsisitiza Mheshimiwa Mbunge kwamba tusaidiane kwa pamoja kufichua wale askari wachache ambao watakuwa wanatuhumiwa ama wanajihusisha na tabia kama hizo zilizokuwa kinyume na maadili ya utendaji kazi wa Jeshi la Polisi.

Name

John John Mnyika

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Kibamba

Primary Question

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:- Kumekuwa na baadhi ya Askari wa barabarani wanaosimamisha magari hasa yale ya safari ndefu wakitokea vichakani (kujificha) na hatimaye wakati mwingine kusababisha ajali:- Je, ni Askari wangapi kama hawa wameshachukuliwa hatua za kinidhamu?

Supplementary Question 3

MHE. JOHH J. MNYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Katika kujibu swali la msingi, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema Serikali iliandaa mkakati maalum wa kudhibiti ajali barabarani na kwamba umetekelezwa kwa kiwango cha ajali kupungua kwa asilimia 43. Sasa Je, Serikali ipo tayari kuleta huo mkakati iliouandaa Bungeni pamoja na taarifa ya utekelezaji Bungeni ili tuweze kupima kama Wabunge ni ukweli ajali zimepungua kwa asilimia 43?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa John Mnyika Mbunge wa Ubungo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleze kwanza kwa ufupi kabisa kuhusiana na mkakati huu. Mkakati huu upo kwa awamu, tulianza mkakati wa miezi sita ambao ulikuwa na lengo la kupunguza ajali kwa asilimia kumi, tukafanikiwa kupunguza ajali kwa asilimia kumi na moja. Tukaja mkakati wa awamu ya pili ambao ulikuwa miezi sita, tuka-target asilimia kumi, tukapunguza ajali kwa asilimia 45 nadhani. Tukaona kwamba tuna haja ya kuongeza sasa malengo tukaweka mkakati wa asilimia 25 kupunguza ajali wa miezi sita vilevile, ambao tulifanikiwa kupunguza ajali kwa asilimia 25. Hivi tunazungumza tupo katika mkakati wa awamu ya nne ambao tumelenga kupunguza ajali kwa asilimia 25. Kwa hiyo asilimia 43 tuliyozungumza ni kwa jumla wake kwa maana ya mwaka mzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niliona nimpe kwanza utangulizi huo aelewe kwamba si mkakati mmoja, ni mkakati ambao tumekuwa tukijipima awamu kwa awamu kupitia Baraza la Usalama Barabarani na mkakati huu upo wazi na Mheshimiwa Mbunge atakapohitaji wakati wowote sisi tutakuwa tayari kumpatia. Tumekuwa tukifanya hivyo kwa sababu malengo ya mikakati hii tunapomaliza tunakuwa tunashirikisha wadau mbalimbali ikiwemo Wabunge, hata yeye mwenyewe Mheshimiwa tulimwalika juzi katika Kongamano letu la Usalama Barabarani ambapo tulizungumzia mkakati huu Dar es Salaam na Wabunge wengine wa Mkoa wa Dar es Salaam wote, lakini bahati mbaya hatukumwona Mheshimiwa Mnyika japokuwa barua niliisaini mimi mwenyewe kwa mkono wangu ili kuonyesha kwamba hili jambo ni jambo shirikishi na tunatambua umuhimu wa kuwashirikisha na tutaendelea kuwashirikisha Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla.