Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Joseph Kizito Mhagama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Madaba

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA (K.n.y MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI) aliuliza:- TPB ni Benki ya Serikali na inamilikiwa na Serikali kwa zaidi ya asilimia 90 lakini Taasisi za Serikali na Mashirika ya Umma yanatumia Benki nyingine katika huduma za Kibenki:- (a) Je, ni nini msimamo wa Serikali katika kutumia huduma za Kibenki? (b) Watumishi wa Serikali na Viongozi wote wa Serikali wanatakiwa kutumia TTCL katika huduma za mawasiliano ya simu. Je, kwa nini Watumishi na shughuli zote za Serikali zisianze kutumia huduma za Kibenki kupitia Benki hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza:

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niipongeze sana benki ya TPB kwa kufanya kazi vizuri na kuendele kujiboresha, nina maswali mawili ya nyongeza ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja ya sababu ya kuanzisha benki zinazosimamiwa na Serikali popote duniani, sababu za kuanzisha Benki za Umma ni kwenda kua-address mapungufu ambayo sekta binafsi, Mabenki Binafsi yameshindwa kuyashughulikia. Miongoni mwa mapungufu hayo ambayo tunayo hapa Tanzania ni kwamba Wajasiriamali wengi wadogo wanashindwa kufanya biashara zao kwa sababu hawana mitaji, ni kwa namna gani Benki hii ya Posta inajitofautisha na benki zingine za kibiashara katika kusaidia Wajasiriamali wadogo nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili swali langu tumeona kwamba Benki ya Kilimo Tanzania haina matawi katika Mikoa mingi na Wilaya nyingi na Wakulima wanakosa mitaji ya biashara ni kwa namna gani sasa Serikali imejipanga kuitumia Benki ya Posta kama Tawi kama tawi la Benki ya Kilimo Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ni jinsi gani TPB inajitofautisha katika kutoa huduma na benki nyingine za biashara, naomba kumpa taarifa kwamba Benki ya TPB kwanza ina Matawi katika Mikoa yote Tanzania na imekwenda katika Wilaya ambazo tunasema ni kama Wilaya za Vijijini ambako Mabenki mengi ya biashara hayajafika, kwa hiyo hilo ni jambo la kwanza walilolifanya kuwafikia wananchi wetu kule walipo. Pia, Benki ya TPB ina mfumo wa kukaa na Wajasiriamali kuwapa mafunzo na kuwapa mikopo ambayo ina riba nafuu ikishirikiana na Benki yetu ya Kilimo Tanzania.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ni jinsi gani inaweza kushirikiana naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Bunge lako Tukufu tayari Benki yetu ya Kilimo ilishafungua matawi yake kwenye Kanda, Kanda ya Mwanza na Kanda ya Kati, tayari wameanza kufanya kazi na sasa wanajiandaa kwenda kufungua Tawi lao Mkoani Mbeya ili kuhudumia Nyanda za Juu Kusini. Wakati tukiendelea kufungua matawi ya Benki yetu ya Kilimo, Benki ya Kilimo pamoja na Benki ya TPB wanashirikiana na kwa mwaka huu wa fedha peke yake wametoa mikopo zaidi ya bilioni 431 kwa wakulima wetu kwenye maeneo yale ambapo TADB haina matawi lakini TPB imeweza kufika.

Mheshimiwa Spika, ni imani yetu sisi kama Wizara tunayosimamia sekta hii kuhakikisha kuwa wananchi wetu wakiwemo wajasiriamali wadogo pamoja na Wakulima wetu wanafikiwa na huduma hizi kupitia Benki hizi za Umma zinazoendeshwa kwa kodi zao.