Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: - Elimu ya Msingi ni muhimu kuwawezesha wahitimu kuzalisha na kuwapatia stadi za maisha lakini wapo wahitimu wa Elimu ya Msingi, Sekondari na Vyuo wasioweza hata kuanzisha bustani za mboga mboga na matunda:- Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha elimu inayotolewa inamwezesha mhitimu kupata ujuzi na stadi za maisha ili aweze kujiajiri?

Supplementary Question 1

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nianze kwanza kumpongeza Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kutoa elimu bure ambayo imewezesha kila mtoto sasa atoke akasome na hakuna dadalea tena nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la msingi nimesisitiza elimu ya msingi kuwezesha wanafunzi kwenda kufanya kazi zao baada ya masomo kwa wale ambao hawataendelea. Naomba kuuliza maswali kwa Serikali, la kwanza, kwa kuwa wanafunzi hao tunaowaona barabarani na nyie mkiwa mashahidi wanatoka nyumbani alfajiri saa kumi na moja na kurudi nyumbani saa kumi na mbili hoi bin taabani, kwa maana muda mwingi wako shuleni na shuleni ndiko wanakoweza kufundishwa, kwa nini sasa katika elimu ya msingi walimu wasiwe na mtaala ambao watafufua zile bustani ndogondogo toka wakiwa wadogo wawe na interest ya kilimo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kipindi cha nyuma tulikuwepo na sekondari za mchepuo, tulikuwa na sekondari ya mchepuo wa kilimo, mchepuo wa biashara, mchepuo wa sayansikimu na kadhalika. Baada ya hayo yaliyotokea hapo katikati na michepuo ile kufutia, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kurejesha tena aina ile ya mitaala ili mwanafunzi akitoka pale pamoja na kulelewa nyumbani na wazazi, kulelewa shuleni, lakini taifa ka kesho liwe bora kama nyie mlio hapa? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shally Raymond, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na umuhimu wa Serikali kurejesha bustani mashuleni, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sehemu kubwa wanafunzi bado wanapata fursa za kujifunza kilimo kidogo kidogo hasa maeneo ya vijijini lakini changamoto wote tunafahamu ni maeneo ya mjini ambapo ardhi ni changamoto kubwa. Ndiyo maana tunaendelea kusisitiza kwamba jamii, familia waisaidie Serikali nao waweze vilevile kutoa stadi hizo kwa vijana, kwa sababu lazima tuseme pia kwamba maisha ya kisasa yanahusika kwa kiasi kikubwa katika kuondoa ari na hamasa ya vijana kujihusisha na vitu kama hivyo. Wazazi wengi wanapenda watoto wao wakacheze na play station, kuangalia TV, video games kuliko kujifunza stadi za maisha. Ndiyo maana tunasema, ndiyo Serikali itaendelea siyo tu kuboresha mitaala lakini kuweka mazingira wezeshi ili wanafunzi waweze kupata hizo stadi za kazi lakini kama nilivyosema ni jukumu letu wote. Kwa hiyo, tunomba tusaidie ili tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kubadilisha mitaala ili turudi nyuma, naomba nichukue mawazo yake, siyo baya tutaendelea kuboresha mitaala yetu ili iweze kutoa elimu bora na yenye manufaa kwenye vijana wetu. (Makofi)

Name

Alex Raphael Gashaza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngara

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: - Elimu ya Msingi ni muhimu kuwawezesha wahitimu kuzalisha na kuwapatia stadi za maisha lakini wapo wahitimu wa Elimu ya Msingi, Sekondari na Vyuo wasioweza hata kuanzisha bustani za mboga mboga na matunda:- Je, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha elimu inayotolewa inamwezesha mhitimu kupata ujuzi na stadi za maisha ili aweze kujiajiri?

Supplementary Question 2

MHE. ALEX R. GASHAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, takribani watoto 115 waliomaliza darasa la saba mwaka jana na kufanya mtihani kutoka Jimbo la Ngara katika Shule ya Msingi Kumnazi walifutiwa mtihani na wazazi wa watoto hao kwa umoja wao walimwandikia Katibu Mkuu Baraza la Mitihani barua ya tarehe 10 Desemba lakini mpaka sasa hivi hawajapata majibu. Watoto na wazazi wamechanganyikiwa ukizingatia ni watoto yatima na wengi wao ni watoto wa maskini. Nini kauli ya Serikali kuhusu suala hili?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwanza swali hili halina uhusiano na swali la msingi ambalo nilikuwa najibu lakini naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gashaza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu barua ambao wazazi wale wameandika kwa Katibu Mtendaji wa Baraza la Mtihani, naomba nifuatilie nijue barua hiyo majibu yake yanatoka lini. Hata hivyo, ifahamike tu kwa umma na kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba ni kosa kujihusisha na uhalifu wa mitihani. Kwa hiyo, pale mtuhumiwa atapobainika kwamba kweli amehusika hatua stahiki zinachukuliwa na hatua hizo inakuwa ni pamoja na kumfutia mtihani na matokeo. Kwa hiyo, ifahamike tu kwamba kwa kweli ni kosa lakini nitaenda kufuatilia halafu nitampa jibu.