Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mwanne Ismail Mchemba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA) aliuliza:- Waendesha pikipiki (bodaboda) nchini wamekuwa wakikamatwa na Askari wa Usalama Barabarani mara kwa mara kwa tuhuma za makosa mbalimbali:- Je, zoezi hili la ukamataji wa waendesha pikipiki limefanikiwa kwa kiasi gani?

Supplementary Question 1

MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza naipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayofanya ya kuhakikisha kwamba usalama wa barabarani unasimamia mazingira yote. Kwa kuwa usalama barabarani wanafanya kazi kubwa na kwa kuwa waendesha bodaboda kwa sasa pamoja na kupunguza ajali, wapo wanaovunja sheria na baada ya kuvunja sheria wao pia wanakuwa vyanzo vya watu kupata ulemavu: Je, Serikali inatoa adhabu gani kali kwa hao ambao wanavunja sheria?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha inasajili bodaboda zote hapa nchini ili kupunguza uhalifu na kupunguza ajali pale inapotokea wale wenye bodaboda wanapokimbia?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, aina ya adhabu zipo kwa mujibu wa Sheria ya Usalama Barabarani lakini inategemea pia aina ya kosa la mhusika. Hata hivyo nikiri kwamba inawezekana adhabu hizo sasa hivi zikawa zimepitwa na wakati, ndiyo maana tupo katika hatua za mwisho za mchakato wa marekebisho makubwa ya Sheria za Usalama Barabarani. Ni imani yetu kwamba sheria hiyo itakapokamilika, inaweza ikasaidia sasa kuweka adhabu ambazo zitawabana zaidi wavunjifu wa sheria za usalama barabarani hususan waendesha bodaboda.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la usajili, nimhakikishie kwamba tupo katika hatua za kuanza mchakato huo tukiamini kwamba utaratibu huo utasaidia sana katika kupunguza malalamiko ya baadhi ya waendesha bodaboda ya uonevu wanaofanyiwa dhidi ya baadhi ya Askari wetu, lakini pia itasaidia sana kuweza kuwadhibiti na kuwakamata pale ambapo wanafanya makosa hayo kwa urahisi na uvunjifu wa Sheria za Usalama Barabarani kwa wanaotumia bodaboda.

Name

Masoud Abdalla Salim

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtambile

Primary Question

MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA) aliuliza:- Waendesha pikipiki (bodaboda) nchini wamekuwa wakikamatwa na Askari wa Usalama Barabarani mara kwa mara kwa tuhuma za makosa mbalimbali:- Je, zoezi hili la ukamataji wa waendesha pikipiki limefanikiwa kwa kiasi gani?

Supplementary Question 2

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika maelezo ya Mheshimiwa Waziri, yaani majibu yake, anasema kwamba ajali zimepungua lakini vifo vimeongezeka.

Mheshimiwa Spika, kwa idadi ya vifo ambavyo wamevitaja kuanzia mwaka 2017, 2018, 2019 hadi Juni inaelekea kwamba jumla ya vifo vilivyotokea ni 1,270. Hawa ni Watanzania, idadi ni kubwa. Mheshimiwa Naibu Waziri tuambie hasa mkakati wa ziada wa mwarobaini ili kukomesha vifo hivi visiendelee tena. Nashukuru sana.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, niliposoma takwimu tokea mwaka 2016 mpaka 2019 kwa ujumla ajali, vifo na majeruhi vyote vinaonekana kushuka, lakini takwimu ambazo nilisema kwamba vifo vinaongezeka ni za kipindi cha Januari mpaka Juni 2019. Kwa hiyo, ni kipengele kimoja na cha kipindi kimoja ambacho tumeona kwamba upande wa vifo umeongezeka, lakini kwa ujumla ajali zimepungua.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeeleza, haya ni mafanikio ya usimamizi wa Sheria ya Usalama Barabarani ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kupunguza ajali za barabarani ambao tumeuandaa kupitia Baraza la Usalama la Taifa kwa maana mkakati huu umegusa katika maeneo mengi. Moja, ndiyo hili eneo ambalo nimezungumza katika jibu langu la msingi kwamba ni kuhakikisha kwamba Askari wetu wanasimamia Sheria ya Usalama Barabarani kwa nguvu zote na kwa mujibu wa sheria.