Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:- (a) Je, ni sababu zipi zinazosababisha matangazo ya Shirika la Habari Tanzania (TBC) hasa upande wa Radio yasisikike kwenye Tarafa za Kitunda na maeneo mengi ndani ya Jimbo la Sikonge? (b) Je, ni lini Serikali itarekebisha tatizo hilo?

Supplementary Question 1

MHE. DEVOTHA M. MINJA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, sote tunatambua kuwa Redio Tanzania inaendeshwa na kodi za Watanzania na kwa sasa ni zaidi ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Redio Tanzania lakini maeneo ya pembezoni haisikiki na watu wanalazimika kusikiliza redio za nchi jirani. Hivi tunakwama wapi? Ni kwa nini TCRA isiondoe vikwazo kwa redio binafsi ili zipewe jukumu la kuhakikisha zinatoa huduma na kuwafikia Watanzania katika maeneo yote nchini? (Makofi)

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa nashukuru, hizi zote ni neema za Mwenyezi Mungu. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Devotha Minja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nitumie fursa hii kumtoa hofu kwamba TCRA kwa maana ya Serikali haijaweka vikwazo kwa redio yoyote ya binafsi kuanzisha vituo vyake vya redio. Mara zote sisi kama Wizara ambao tunasimamia masuala yote ya habari lakini kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Mawasiliano, tumekuwa tukisisitiza kwamba milango iko wazi kwa mtu na taasisi yoyote ambayo inataka kuanzisha redio waweze tu kufuata zile taratibu ambazo zinatakiwa katika kuanzisha redio hizo.

Mheshimiwa Spika, vilevile, sisi kama Wizara ambao tunasimamia masuala ya habari nchini Tanzania tumekuwa tukihakikisha kwamba maeneo yote ya mipakani yanafikiwa na usikivu wa Redio yetu ya Tanzania. Katika kuthibitisha hilo, kwenye jibu langu la msingi nimesema wazi kwamba katika bajeti ya mwaka 2016/2017, TBC ilifanya uwekezaji mkubwa sana katika maeneo yote ya pambezoni ikiwemo katika wilaya zote ambazo zipo mipakani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama Serikali tunatambua concern yake kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuboresha usikivu wa TBC pamoja na Redio Tanzania katika maeneo yote ya mpakani.

Mheshimiwa Spika, ahsante.