Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ester Amos Bulaya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. BULAYA aliuliza:- Kumekuwepo na matukio ya mara kwa mara ya wananchi wa Vijiji vya Guta, Tairo, Nyamtwali na Njabeu kukamatwa na kuliwa na mamba; hadi swali hili linaandikwa, jumla ya watu watatu wameliwa na wengine kumi wamejeruhiwa. Je, Serikali inajipangaje ili kuokoa maisha ya wananchi kutokana na hatari kubwa ya mamba hao?

Supplementary Question 1

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika kwa baadhi ya majibu ya uongo ambao Mheshimiwa Naibu Waziri ameyajibu. Mimi ndio
Mbunge wa Jimbo husika na kuna mwananchi wangu nimemhudumia katika Hospitali ya DDH. Aliyekupa hizo taarifa kamwulize vizuri, amekuongopea.
Mheshimiwa Naibu Spika, naenda sasa kwenye swali. Sheria ya Kazi Na. 6, mtu anapokufa kazini, analipwa fidia shilingi milioni 10. Hawa wananchi wangu walikuwa kazini, mbali na kwamba wamejiajiri wenyewe, mwalipe fidia, siyo kifutajasho cha laki moja moja. (Makofi)
Swali la pili; Mheshimiwa Waziri, tatizo la mamba katika vijiji nilivyokwambia ni kubwa sana, hata kwa kaka yangu kule Mheshimiwa Kangi, wananchi wanavua kienyeji kwa kutumia kuku. Lini Wizara yako itapeleka wataalam mwavue? Wananchi wangu wanakufa kila siku wanakuwa vilema halafu unatoa majibu mepesi hapa!

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba umesema swali la kwanza pengine lingejibiwa na Waziri wa Sheria lakini napenda kutoa sehemu ya majibu.
Mhehimiwa Naibu Spika, Serikali inafanya kazi zake kwa kutumia mfumo wake. Kwa hiyo, taarifa ambazo zimo katika majibu niliyoyatoa zimetoka kwenye Halmashauri ya Bunda na vyombo vya Serikali vilivyopo kule. Kwa hiyo, kwa kuwa Mheshimiwa Ester Bulaya ni Mjumbe wa Halmashauri ya Bunda, anaweza kwenda kuwahoji waliotoa taarifa hizi ambao ni Halmashauri inayohusika kwamba kwa nini wameleta majibu ya uongo?
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu fidia kwamba Serikali inalipa kifuta jasho au kifuta machozi na siyo fidia; na Mheshimiwa Mbunge angependa badala yake tulipe fidia, kwa sababu kiwango cha shilingi laki moja ni kidogo; nchi hii inaendeshwa kwa mujibu wa sheria. Hakuna namna yoyote ambayo unaweza kuendesha nchi bila kufuata sheria, kanuni na taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ulipaji wa kifuta jasho na kifuta machozi ni utaratibu uliopitishwa kwa mujibu wa sheria ambayo imepitishwa na Bunge hili. Iwapo itaonekana kwamba utaratibu huo haufai kwa namna yoyote ile, ni wajibu wa Waheshimiwa Wabunge kwa niaba ya wananchi, Mheshimiwa Ester Bulaya akiwa mmoja wao kuleta mapendekezo ya kufanya mapitio upya ya Sheria hii na kama itafaa, pengine Serikali inaweza ikaanzisha utaratibu mwingine badala ya huu.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuongezea jibu zuri ambalo limetolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwanza napenda niseme kwamba Wizara itafuatilia kuona kama kuna taarifa zaidi ya zile ambazo tunazo ili tuweze kuzishughulikia kama ambavyo tumeshughulikia sheria hizo nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, mimi sio Mwanasheria, lakini najua kwa sababu nilifanya kazi kwenye Wizara ya Kazi, kwamba hakuna Sheria ya Kazi ambayo inafidia raia wakati yuko kwenye shughuli zake. Sheria ile ya Kazi ni ya wafanyakazi kama ambavyo inajulikana kwenye sheria ile.