Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. DEVOTHA M. MINJA) aliuliza:- Askari wa Jeshi la Polisi na Magereza wanaishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi ukilinganisha na kazi zao wanazofanya kwa jamii. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaboreshea makazi.

Supplementary Question 1

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa majibu ambayo tumeyapata kwa swali hili, kidogo yana mchanganuo ambao unafaa tofauti na mara ya mwanzo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niulize maswali yangu mawili ya nyongeza. Dhiki katika Jeshi la Magereza ni uzembe kwa sababu kwa maoni yangu Jeshi hili ni Jeshi tajiri, Jeshi hili lilikuwa na Gereza la Kilimo Songwe ambalo lilikuwa linafanya kazi vizuri sana, Gereza la Karanga lilikuwa na kiwanda kizuri sana cha viatu, Gereza la Ukonga lilikuwa na kiwanda kizuri sana cha nguo; lakini tender zinatolewa kununua nguo za Magereza na za Polisi, tender zinatolewa kununua viatu vya Polisi na Magereza. Kwa nini, Serikali isiboreshe viwanda vya Jeshi hili, ili Jeshi likafanye biashara na likaweza kutatua matatizo yake pamoja na matatizo ya nyumba na hata kuisaidia Serikali, badala yake inatoa kazi ambazo Jeshi hili linaweza likazifanya kwa watu wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, nashukuru kwa mchanganuo uliotolewa. Naomba kumuuliza Waziri, kwa kuwa Askari Magereza katika Jimbo langu pale Rombo wanaishi katika nyumba zinazoitia aibu Serikali kwa kweli, wanaishi kwenye mabanzi. Je, Waziri yupo tayari kuandamana na mimi akakague nyumba hizo na kwa sababu hiyo, hizi zilizotengwa 390 angalau chache zianze kujengwa Rombo kwa ajili ya kunusuru makazi ya wale Askari pale Rombo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza limepanga kuongeza uzalishaji wa mapato ya kilimo, ushonaji na ufugaji. Kwa hiyo, msingi wa swali lake kwamba Jeshi la Magereza limezembea siyo sahihi, kuna mipango kabambe tu ya kuhakikisha kwamba Jeshi la Magereza linajitegemea kwa chakula, lakini pia linaendeleza ujuzi na rasilimaliwatu ilizokuwa nazo katika kuhakikisha kwamba linachangia juhudi za Serikali za kuweza kuifanya sekta ya viwanda kuchukua sehemu kubwa katika uchumi wa nchi yetu katika miaka inayokuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia utaratibu huo Jeshi la Magereza limeandaa andiko ambalo linaainisha miradi minane. Uzalishaji wenye matokeo makubwa ya haraka (quick win projects) na limeshawasilishwa Serikalini ili kuweza kupata fedha. Miradi hiyo ambayo ni ya kokoto Msalato; unenepeshaji wa ng‟ombe wa nyama Mbigili na Ubena; uzalishaji wa mafuta ya alizeti Ushora, Kongwa na Msalato; ushonaji wa viatu Ukonga na Karanga Moshi ambako ni kwa Mheshimiwa Selasini. Halafu kuna mradi wa samani ambao uko Arusha; kilimo cha umwagiliaji Idete Morogoro na kuimarisha kikosi cha ujenzi ili kiweze kumudu na kufanya kazi kubwa za ukandarasi.
Pia Jeshi hilo limeandika mpangokazi wa kujitosheleza kwa chakula ambalo pia limeshawasilishwa Serikalini ili kupata fedha za uendeshaji. Kwa hiyo, Jeshi linatekekeza sera ya uwezeshaji kwa kuingia ubia pia na taasisi mbalimbali binafsi kupitia utaratibu wa PPP ili kupata mitaji ya kuongeza uzalishaji. Mpaka sasa Jeshi limeshaingia ubia na kampuni ya Tabin ya Uturuki kwa ajili ya kutekeleza kilimo cha mpunga Gereza la Kigongoni. Pia limeainisha maeneo yenye madini na kupata leseni ya uchimbaji karibu 181, hatua za kutangaza maeneo hayo kwa ajili ya uwekezaji zinafanywa. Hilo nadhani lilikuwa ni swali lake la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, ametaka kujua kuhusiana na Kilimanjaro. Kilimanjaro tuna aina mbili, mbali ya ile miradi ambayo nimeizungumza, kuhusiana na huo ujenzi wa nyumba 3,500, lakini pia kuna utaratibu ambao Jeshi la Magereza linaenda nao, kwa kutumia rasilimali zilizopo katika maeneo husika. Kwa Mkoa wa Kilimanjaro tayari nyumba karibu 38 zimejengwa kupitia mradi huo. Kinachofanyika ni kwamba tunatumia rasilimali za nguvukazi zilizopo jeshini pamoja na ujuzi tulionao kuweza kujenga nyumba hizi kufikia katika level ya kuezeka halafu baadaye kupitia fedha za bajeti tunafanya finishing. Kwa hiyo, kupitia utaratibu huo kwa Mkoa wa Kilimanjaro tumeshajenga nyumba 38.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niko tayari kuambatana na Mbunge wakati wowote kwa ajili ya kwenda kuhakikisha kwamba tunatembelea miradi hii na mipango mingine ambayo atakuwa nayo Mheshimiwa Mbunge na tutashirikiana kwa pamoja. Tunapenda Wabunge wa aina yake ambao wako tayari katika kuchangia maendeleo ya nchi yetu.