Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Primary Question

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kufufua zao la kahawa Wilayani Lushoto?

Supplementary Question 1

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Ni kweli kitalu kiko tayari na wakulima wanaendelea kupata miche ya kahawa. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa zao la kahawa ni zao ambalo linaingiza fedha nyingi za kigeni: -

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha zaidi zao hili la kahawa hapa nchini?

(b) Je, ni lini Serikali itaruhusu bei ya zao la kahawa kuamuriwa na nguvu ya soko?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na swali la kwanza la kuboresha na kuhakikisha kwamba tunatafuta masoko ya uhakika. Ni dhamira ya serikali ya awamu ya sita kuhakikisha kwamba zao la kahawa linaendelea kuwa na mchango mkubwa katika kuingiza fedha za kigeni na kubadilisha maisha ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa tunaendelea na kuitangaza kahawa yetu nje ya mipaka ya Tanzania kwa sababu wanunuzi wakubwa wanatoka nje ya mipaka ya Tanzania. Tunashirikiana na Balozi zetu mbalimbali na kupitia matamasha na maonesho mbalimbali tumekuwa tukiitangaza kahawa yetu na jambo hili limetuletea tija kubwa sana. Nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba tunaweka miundombinu wezeshi ili zao hili liweze kupata soko la uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili la kuhusu bei ya kahawa kuamuliwa na nguvu na soko. Mwenendo wa masoko rejea ya kahawa duniani ndiyo ambayo huwa yanaamua bei ya kahawa. Masoko haya ni masoko ya New York kwa kahawa ya arabika na Euronex Uingereza kwa ajili ya robusta. Sisi kama Serikali tumehakikisha kwamba mara zote tunahakikisha wakulima wetu kupitia taarifa hizi wanapata taarifa sahihi na mwisho wa siku waweze kupata bei ambayo itamnufaisha. Kwa hiyo kama Serikali tumeacha nguvu hiyo ya soko iamue, lakini tunawasaidia wakulima wetu kuzalisha kahawa bora ambayo itasaidia pia kuongeza tija katika Soko hilo la Kimataifa. (Makofi)