Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: - Je, Utekelezaji wa mradi wa Mtwara Corridor umefikia hatua gani?

Supplementary Question 1

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Reli ya Kutoka Mtwara mpaka Mbamba Bay ni miongoni mwa miradi midogo iliyopo katika Mradi huu mkubwa wa Mtwara Corridor. Serikali imesema itatekeleza mradi huu kwa ubia. Mimi nataka kujua kwa nini Serikali isitekeleze mradi huu yenyewe ikizingatia umuhimu wake kuliko kusubiria ubia ambao hauna uhakika utapatikana lini?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, mwaka 2004 Lilongwe – Malawi kulisainiwa mkataba wa utekelezaji wa Mradi huu wa Mtwara Corridor na Tanzania inatakiwa iitishe Mkutano ili kutathmini utekelezaji wa mradi huu umefikia hatua gani? Mpaka leo Tanzania haijaitisha: Nataka kujua, ni lini Serikali ya Tanzania itaitisha mkutano huo wa nchi nne; Msumbiji, Malawi, Zambia na Tanzania yenyewe ili kutathmini mradi huu umefikia hatua gani kwa sababu ni mradi muhimu sana katika mikoa ya kusini?

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya uamuzi wa kuzishirikisha sekta binafsi ili kuongeza tija. Pia, kwa sababu Serikali ina commitment nyingi, inaweza ikachelewa kupata fedha kwa ajili ya huu mradi. Hata hivyo, kuna makampuni zaidi ya manne kutoka China, South Africa, Australia pamoja na Marekani, ambao wameonesha nia ya kuwekeza katika mradi huu wa ubia, ukizingatia kwamba eneo hili tayari ni potential kubwa. Uwepo wa makaa ya mawe pamoja na chuma unasababisha wawekezaji hawa waje. kwa sababu tayari mzigo upo metric ton zaidi ya milioni 428 ambapo tunaweza tukachimba zaidi ya miaka 100. Kwa hiyo, sekta binafsi tayari imeonesha utayari huo. Kwa hiyo, tutaendelea kuwa-engage ili mradi huu uweze kuanza mara moja.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anataka kujua ni lini sasa Mkutano wa Wakuu wa Nchi utaitishwa. Tarehe 15 ya Mwezi wa Sita kutakuwa na mkutano wa wadau wote wa sekta na Wizara ya Madini, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Uchukuzi, wadau kutoka sekta binafsi pamoja na taasisi zote za Serikali hususani TRA, MSCL, TPA, RAS Mtwara, RAS Lindi na Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara na Lindi mnakaribishwa kwa ajili ya kujadili jambo hili kama maandalizi ya kuzi–engage nchi zingine za Msumbiji pamoja na Malawi, ahsante.