Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:- Je, lini Kituo cha Afya Kata ya Kafita na Zahanati ya Kijiji cha Nyijundu zitafunguliwa na kupelekewa vifaa baada ya ujenzi kukamilika?

Supplementary Question 1

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza naishukuru Serikali kwa kupeleka fedha zaidi ya shilingi milioni 240 kwenye vituo hivyo vya afya, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa tuna upungufu wa wahudumu wa afya kwenye vituo vya afya ikiwemo Kafita, Nyijundu, Kalumwa na Nyangh’wale na zahanati zote za Jimbo la Nyang’hwale; je, Serikali iko tayari kutupelekea wahudumu wa afya ili kuweza kukidhi mahitaji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa pamoja na kwamba vituo vya afya vimejengwa vingi lakini bado tuna uhitaji wa ujenzi wa kituo cha afya kwenye Kata ya Busolwa; je, Serikali iko tayari kutujengea kituo cha afya kwenye Kata ya Busolwa?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Amar kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napokea shukrani zake kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka fedha nyingi za vifaa tiba katika Jimbo la Nyangh’wale na nchi nzima kwa ujumla. Kuhusu upungufu wa watumishi, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote tumekuwa mashahidi, katika kipindi cha miaka hii miwili Serikali imeajiri watumishi wa kada mbalimbali za afya zaidi ya 17,000 na kuwapeleka katika vituo vyetu vipya pamoja na vya zamani ambavyo vinaendelea kutoa huduma. Kwa hiyo zoezi hili ni endelevu, ajira zitaendelea kutolewa kwa awamu ili kuhakikisha kwamba vituo hivi vinaendelea kupata watumishi wa kutosha na kutoa huduma bora kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa swali la pili linalohusiana na Kituo cha Afya cha Busolwa, Serikali imeshaweka mkakati wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati katika maeneo ya kimkakati, tukizingatia umbali kutoka kituo cha karibu zaidi, idadi ya wananchi katika maeneo hayo na aina ya jiografia ya eneo husika. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya tathmini kuona Kata ya Busolwa kama inakidhi vigezo, na kama inakidhi vigezo tutaanza na mapato ya ndani ya Halmashauri na baadaye Serikali itaona uwezekano wa kuongeza fedha kwa ajili ya kukamilisha, ahsante sana. (Makofi)

Name

Aysharose Ndogholi Mattembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:- Je, lini Kituo cha Afya Kata ya Kafita na Zahanati ya Kijiji cha Nyijundu zitafunguliwa na kupelekewa vifaa baada ya ujenzi kukamilika?

Supplementary Question 2

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itamalizia Kituo cha Afya cha Kata ya Kidaru katika Jimbo la Iramba, hasa ukizingatia watu wake wako pembezoni na hivyo hutembea umbali mrefu kufuata huduma hizo za afya?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali imeanza kujenga kituo cha afya ambacho amekitaja ambacho kipo katika Jimbo la Iramba, na sisi tutahakikisha kituo kile kinakamilika. Ujenzi wa vituo hivi vya afya unakwenda kwa awamu, tuna awamu ya kwanza, ya pili na ya tatu. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba Serikali itatoa kipaumbele kutafuta fedha ili tukamilishe ujenzi wa kituo hiki cha afya.

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:- Je, lini Kituo cha Afya Kata ya Kafita na Zahanati ya Kijiji cha Nyijundu zitafunguliwa na kupelekewa vifaa baada ya ujenzi kukamilika?

Supplementary Question 3

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Mji wa Mafinga imejenga Kituo cha Ifingo na Kituo cha Bumilayinga. Hata hivyo vituo hivi havina huduma kwa ajili ya kulaza akina baba, akina mama na watoto isipokuwa tu kina jengo la mama na mtoto. Je, Serikali iko tayari kutusaidia na kuhakikisha tunapata hizo facilities?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliweka mpango wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati kwa awamu, na katika awamu ya kwanza ilitoa shilingi milioni 500. Kipaumbele ilikuwa ni majengo ya OPD, Maabara, Jengo la Mama na Mtoto pamoja na majengo ya upasuaji na kichomea taka. Hata hivyo, vituo vyote hivi ambavyo vimejengwa bado vinakosa huduma ya wodi ya wanaume, wanawake na wodi ya watoto. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali itaendelea kwa awamu zinazofuata kujenga wodi kwa ajili ya kulaza wanaume, wanawake na watoto ikiwemo katika Kituo hiki cha Ifingo pamoja na Bumilayinga katika jimbo la Mafinga.