Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 42 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 374 2022-06-10

Name

Tumaini Bryceson Magessa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA kwenye vijiji zaidi ya 40 Busanda?

Name

January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Answer

WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tumaini Bryceson Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Busanda lina jumla ya vijiji 83 ambapo kati ya vijiji hivyo vijiji 40 vimefikiwa na miundombinu ya umeme na vijiji 43 havina umeme hivyo vimeingizwa katika Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili katika Mkoa wa Geita ulikumbwa na changamoto iliyotokana na mkandarasi wa kwanza ambaye ni M/s Samheung Electric Power Company Limited aliyeshinda zabuni ya kutekeleza mradi katika Wilaya za Nyang’hwale, Mbogwe na Geita, Mkoa wa Geita kushindwa kuwasilisha dhamana ya kutekeleza kazi yaani performance guarantee ndani ya siku 28 kwa mujibu wa Sheria ya Ununuzi.

Mheshimiwa Spika, hali hii ilipelekea wakala kuanza upya taratibu za ununuzi wa mkandarasi wa kutekeleza mradi huu katika Mkoa wa Geita ambapo kampuni ya M/S CRJE-CTCE Consortium ilishinda zabuni hiyo. REA na mkandarasi waliingia mkataba mpya mwezi Januari, 2022 wa kutekeleza mradi huu unaotarajia kukamilika mwezi Julai, 2023. Kwa sasa mkandarasi huyo anaendelea na utekelezaji wa mradi huo kwa gharama ya shilingi bilioni 25.4 katika Mkoa wa Geita na Busanda ikiwemo.