Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 44 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 392 2022-06-14

Name

Nancy Hassan Nyalusi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NANCY H. NYALUSI aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani za kukabiliana na athari mbalimbali za kiuchumi zinazotokana na hali ya kisiasa duniani?

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante, na kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inafuatilia kwa karibu athari na fursa za kiuchumi na kijamii zinazosababishwa na hali ya kisiasa duniani ikiwemo vita kati ya Urusi na Ukraine. Aidha, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na: -

(i) Kufanya tathmini ya athari za kiuchumi na jamii zinazotokana na vita ya Urusi na Ukraine kwa Tanzania;

(ii) Serikali kutoa ruzuku ya shilingi bilioni 100 kwa ajili ya kupunguza bei ya mafuta kwa kipindi cha kuanzia Juni 1, 2022;

(iii) Kuruhusu wafanyabiashara wenye uwezo wa kuleta mafuta kwa bei nafuu ili kuhakikisha uwepo wa mafuta nchini. Mpango huu unatarajiwa kupunguza bei ya mafuta kuanzia mwezi Agosti 2022;

(iv) Kuhamasisha wafanyabiashara kuagiza ngano kutoka nchi nyingine zinazozalisha ngano ikiwemo Afrika Kusini, Canada, Australia, Uswiss na Ujerumani;

(v) Kuhamasisha uwekezaji wa viwanda vya kuzalisha mbolea nchini ambapo kutokana na uhamasishaji huo, kampuni ya Itracom Fertilizers Limited kutoka Burundi inaendelea na ujenzi wa kiwanda mkoani Dodoma. Kiwanda hicho kitakapokamilika kinatarajiwa kuzalisha tani 500,000 kwa mwaka.

(vi) Serikali kuendelea kutekeleza mikakati mahususi ya kukuza utalii wa ndani na kikanda kupitia fursa za Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na Kamisheni ya Utalii ya Shirika la Utalii Duniani kwa Kanda ya Afrika.

(vii) Kuimarisha sekta ya uzalishaji ikiwemo kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na tathmini ya hatua mbalimbali zinazopaswa kuchukuliwa kwa kila sekta ili kukabiliana na athari za kiuchumi na kijamii zinazotokana na hali ya kisiasa duniani ikiwemo vita ya Urusi na Ukraine, ahsante.