Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 13 Sitting 10 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 147 2023-11-10

Name

Jesca Jonathani Msambatavangu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Iringa Mjini

Primary Question

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kugawa mizinga ya nyuki ili kubadili shughuli za kiuchumi zinazoharibu mazingira kama kukata miti na mkaa Iringa?

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathani Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ugawaji wa mizinga na vifaa vingine ni mojawapo ya mikakati ya Serikali katika jitihada za kuwezesha makundi mbalimbali ya kijamii kushiriki katika shughuli za ufugaji wa nyuki hapa nchini. Zoezi la ugawaji wa mizinga lina lengo la kuchochea ufugaji nyuki kwa jamii hasa zile zinazoishi jirani na maeneo yaliyohifadhiwa ili ziweze kujipatia kipato na kuachana na shughuli zinazoharibu mazingira kama kukata miti na kuchoma mkaa.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuimarisha uhifadhi wa maeneo mbalimbali ambapo kupitia Mradi wa REGROW imetoa elimu ya Ufugaji nyuki kwa jamii ya Tungamalenga na kwa mwaka wa fedha 2023/2024 imepanga kuwagawia mizinga 50 kwa kikundi cha Subira kilichopo Wilaya ya Iringa. Vilevile elimu ya ufugaji nyuki imeendelea kutolewa kwa jamii zinazozunguka hifadhi ambapo kupitia elimu hiyo wananchi wamefundishwa namna bora ya kufanya shughuli za ufugaji nyuki kwa tija.

Mheshimiwa Spika, mathalan kwa mwaka wa fedha 2022/2023, Wizara ilitoa mizinga 269 yenye thamani ya shilingi milioni 26.9 kwa vikundi 19 vya wafugaji wa nyuki katika Wilaya za Iringa, Kilolo na Mufindi. Vilevile Mfuko wa Misitu Tanzania umetoa ruzuku ya shilingi millioni 20 kwa vikundi viwili vya ufugaji Nyuki vilivyopo Wilaya ya Iringa. Pia, wadau wa maendeleo wametoa mizinga 260 kwa wafugaji nyuki katika Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo, itaendelea kutoa elimu ya uhifadhi na mbinu bora za ufugaji nyuki ili jamii iweze kufuga nyuki kibiashara. Aidha, Mfuko wa Misitu Tanzania umekuwa ukitoa tangazo na kupokea maombi ya ruzuku zitolewazo kwa wadau wa misitu na ufugaji wa nyuki. Hivyo, Mfuko unaendelea kupokea maombi ambayo yanachakatwa ili waombaji waweze kunufaika na ruzuku hizo ikiwemo kupatiwa mizinga ya kufugia nyuki.