Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 8 Natural hazards and Disasters Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu na Bunge 127 2024-02-02

Name

Zahor Mohamed Haji

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwera

Primary Question

MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI aliuliza: -

Je, zipi athari za mvua zilizonyesha Novemba, 2023 na Serikali imejipangaje kuzuia athari hizo kujirudia?

Name

Ummy Hamisi Nderiananga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zahor Mohamed Haji, Mbunge wa Jimbo la Mwera, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha kuanzia Mwezi Oktoba, 2023 hadi sasa, tumeshuhudia mvua kubwa ambazo zimenyesha katika maeneo mbalimbali nchini. Mvua hizo, zimeleta athari mbalimbali ikiwemo mafuriko, maporomoko ya ardhi, magonjwa ya milipuko kwa binadamu ikiwemo kipindupindu, matukio ya radi na matukio ya upepo mkali ambayo yamesababisha uharibifu wa miundombinu, madhara ya kiafya, kiuchumi, kijamii na upotevu wa mali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na athari hizi, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na hali ikiwemo kuandaa Mpango wa Taifa wa Dharura wa Kukabiliana na Madhara ya El-Nino kwa kipindi cha Septemba, 2023 mpaka Juni, 2024. Vilevile, kuzijengea uwezo Kamati za Usimamizi wa Maafa katika mikoa 18 nchini, kufuatilia mwenendo wa majanga, kutoa tahadhari kwa umma kupitia Kituo chetu cha Oparesheni na Mawasiliano ya Dharura na kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa kupitia utekelezaji wa mikakati na mikataba ya Kikanda na Kimataifa, ikiwemo Mkakati wa Kimataifa wa Sendai wa Upunguzaji wa Athari za Maafa wa Mwaka 2015/2030; na Mkataba wa Makubaliano wa kuanzisha Kituo cha Huduma za Kibinadamu na Oparesheni za Dharura cha Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, yapo madhara ambayo kwa msingi wake wa kuwa majanga ya asili pale yanapotekea hata athari zake hujirudia. Hivyo, Serikali imeendelea kujumuisha athari za majanga hayo katika mpango wa uzuiaji na urejeshaji wa hali pale inapobidi, ahsante.