Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 41 Good Governance Ofisi ya Rais TAMISEMI. 345 2016-06-13

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI (K.n.y. MHE. RUTH H. MOLLEL) aliuliza:-
Mheshimiwa Rais amepunguza idadi ya Wizara kutoka 23 hadi 18 ili kupunguza gharama za uendeshaji:-
Je, ni kiasi gani cha fedha za walipa kodi zilizookolewa kwa kuwa na idadi ndogo ya Wizara.

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Hiyob Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya Mheshimiwa Rais ya kupunguza Wizara kutoka Wizara 28 hadi 18 ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi yake, ya kupunguza gharama za uendeshaji na ukubwa wa Serikali aliyoitoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na katika Hotuba yake wakati akizindua Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lengo likiwa ni kuboresha huduma kwa wananchi wetu kwa kuelekeza matumizi makubwa ya Serikali katika huduma za kijamii, kama vile afya, elimu, maji, miundombinu na mawasiliano pamoja na miradi ya maendeleo.
Uundwaji wa Serikali ya Awamu ya Tano bado unaendelea, kwa sasa Serikali inafanya uchambuzi wa kina wa majukumu ya kila Wizara, na taasisi zake ili kuainisha majukumu ambayo ni muhimu kuendelea kutekelezwa na Serikali na taasisi zake au la na kuchukua hatua stahiki. Uchambuzi huu utaiwezesha Serikali kubaini majukumu yanayofanana ndani ya taasisi, lakini yanatekelezwa na kitengo au Idara zaidi ya moja, au majukumu yanayofanana, lakini yanatekelezwa na taasisi zaidi ya moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hili pia litawezesha kubaini, kama idara au vitengo ndani ya Wizara na taasisi zake, vina majukumu ya kutosha ya kuhalalisha uwepo wake. Kukamilika kwa uchambuzi huu, ndio itakuwa msingi kwa Serikali kuuhisha miundo ya mgawanyo wa majukumu wa Wizara na taasisi zake na hivyo kujua gharama halisi, zitakazotokana na kupunguzwa kwa Wizara kutoka 28 hadi kufikia 18.