Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 6 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 68 2016-02-02

Name

James Kinyasi Millya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Primary Question

MHE. JAMES K. MILLYA aliuliza:-
Madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu katika Wilaya ya Simanjiro, tofauti na dunia inavyopotosha kuwa madini hayo yanatoka India na Kenya, ambako huenda Serikali hizo huwapa mitaji wafanyabiashara wao:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia Watanzania wanaofanya biashara ya Tanzanite kwa kuwapatia mitaji ili waweze kushindana na wafanyabiashara wa nje?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa James Kinyasi Millya, Mbunge wa Simanjiro, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu katika Wilaya ya Simanjiro. Maelezo kwamba yanapatikana sehemu nyingine duniani, ni upotoshwaji mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sina uhakika kwamba Serikali za India na Kenya zinawasaidia wafanyabiashara wa Tanzanite katika nchi zao kwa kuwapa mitaji ili kufanya biashara na ushindani wa nchi za nje. Lakini Serikali ya Tanzania inawasaidia wafanyabiashara wa madini wakiwemo wa Tanzanite kwa kuwawekea mazingira mazuri ya kibiashara kwa kuhakikisha kwamba wanakuwa na leseni halali za brokers au dealers ili wafanye biashara zao kihalali kwa kutumia mitaji yao ya kifedha na pia kwa kuzingatia sheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na Kituo cha Arusha International Conference Center ina mpango wa kujenga jengo katika Jiji la Arusha kwa ajili ya biashara ya madini ambalo litakuwa na miundombinu inayotakiwa kwa ajili ya biashara hiyo. Lengo ni kuwahakikishia wafanyabiashara wa madini wanauza madini yao nchini kwa usalama na uhakika zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikiandaa maonesho ya madini ya vito nchini maarufu kama Arusha Gem Fair yanayofanyika kila mwaka jijini Arusha. Lengo ni kuwaunganisha wafanyabiashara wa madini nchini pamoja na wale wa Kimataifa ili kujitangaza kibiashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kuwa biashara ya madini inaenda sambamba na shughuli zinazofanywa na wachimbaji wa madini wadogo wadogo. Hivyo, Serikali imekuwa ikiwasaidia wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kuwapatia ruzuku, ambapo kwa mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara ilitoa ruzuku ya jumla ya shilingi bilioni 7.2 kwa wachimbaji wadogo. Kadhalika ilitoa ruzuku hiyo kwa watoa huduma migodini, wakiwemo wanaofanya biashara ya Tanzanite.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale ambao hawakukidhi vigezo, wamepewa barua kueleza sababu za kutokidhi vigezo hivyo na wanakaribishwa kuomba ruzuku tena mara watakapopata fedha na kutoa tangazo la kibiashara kwa ajili ya ruzuku ya awamu inayofuata.