Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

James Kinyasi Millya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Primary Question

MHE. JAMES K. MILLYA aliuliza:- Madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu katika Wilaya ya Simanjiro, tofauti na dunia inavyopotosha kuwa madini hayo yanatoka India na Kenya, ambako huenda Serikali hizo huwapa mitaji wafanyabiashara wao:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia Watanzania wanaofanya biashara ya Tanzanite kwa kuwapatia mitaji ili waweze kushindana na wafanyabiashara wa nje?

Supplementary Question 1

MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu yasiyoridhisha, ni dhahiri kwamba Serikali haijajipanga kuwasaidia wachimbaji wadogo wadogo. Kinachonisikitisha zaidi, eti Serikali imejipanga kwenye kituo cha madini, kitakachoanzishwa na AICC na Wizara, kijengwe Arusha. Mjini Sri-Lanka, geuda sapphire...

MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Naibu Spika, Sri-Lanka. Kwa kuwa Sri-Lanka imejipanga kwenye geuda sapphire red stone, kwenye Mji wa Ratnapura; Madagascar Afrika, kwa nini Serikali ya Tanzania isijipange kati ya Mererani na Naisinyai, ianzishe kituo hiki ili heshima hii ipewe Simanjiro? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kati ya Disemba na Januari, Wizara ikishirikiana na Jeshi la Polisi, wamewakamata vijana wasio na ajira wa Simanjiro kati ya Mererani na Arusha, wamenyanganywa madini yao, vijana hawa hawajasoma, wanajitafutia maisha. Ni lini Serikali inayojitapa inatafutia vijana ajira, itawasaidia vijana hawa kupata ajira na kutowanyanyasa kwenye nchi yao? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Prof. Sospeter Mwijarubi Muhongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Vijijini

Answer

WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, siyo kweli kwamba Serikali haijawasaidia wachimbaji wadogo. Kama ingekuwa hivyo, kama kweli wachimbaji wadogo wasingefaidika, kwenye Kikao chao cha Geita, wasingenichagua mimi niwe mlezi wao Kitaifa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba ruzuku ya kwanza tuliyoitoa, sisi Wizara ndiyo tuliitafuta, tuliitoa kwa vikundi zaidi ya 10 na kila Kikundi kilipewa ruzuku ya dola 50,000. Awamu ya Pili, tumetoa ruzuku ambayo kiwango cha juu kabisa ni dola 100,000 ambavyo ndiyo Naibu Waziri alikuwa anasema, tumetoa kwenye vikundi 111.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Shirika la Madini Tanzania (STAMICO) limefungua desk, wameweka Idara kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Sasa hivi tunavyofanya ni kwamba eneo la wachimbaji wadogo likitengwa (geological survey). Wakala wa jiolojia hapa anaenda kwa gharama ya Serikali, wanafanya utafiti kabla hatujawapatia wachimbaji wadogo maeneo. Kwa hiyo, kazi inafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi kwenye Tanzanite. Ndugu yangu Mheshimiwa Mbunge, tumejadili naye na kwa heshima kabisa, nimekusanya watu kesho ofisini na mwenyewe anajua. Namleta Kamishna, naleta watu kutoka Arusha, waje wakae naye kwanza wampe somo la mambo ya biashara ya Tanzanite. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumepanga naye anafahamu hivyo. Mbali na hapo Mheshimiwa Mbunge atakubali kwamba wakati sisi tunatengeneza mambo ya Tanzanite, watu walilalamika wakasema wamejitokeza Watanzania wapewe huo mgodi. Nawe unajua kuanzia jana wananchi wamegoma, hawawataki hawa wawekezaji mliokuwa mnawashabikia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutaendelea kutatua suala la Tanzanite kwa jinsi linavyotatuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mifano aliyoitoa Mheshimiwa Mbunge ya Sri-Lanka na Madagascar, kwa heshima zote siyo kweli. Kwa sababu mimi nimeenda Madagascar mara nyingi sana; na nilikuwa nashughulikia gem stones za Madagascar na Sri-Lanka. Ukienda Madagascar utakuta badala ya vijana kuuza karanga na njugu, wao wanauza gemstones wamezichonga, wameweka kwenye kama viberiti. Huko labda ndiko tutakapokwenda. (Kicheko/Makofi)

Name

Mussa Azzan Zungu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ilala

Primary Question

MHE. JAMES K. MILLYA aliuliza:- Madini ya Tanzanite yanapatikana Tanzania tu katika Wilaya ya Simanjiro, tofauti na dunia inavyopotosha kuwa madini hayo yanatoka India na Kenya, ambako huenda Serikali hizo huwapa mitaji wafanyabiashara wao:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia Watanzania wanaofanya biashara ya Tanzanite kwa kuwapatia mitaji ili waweze kushindana na wafanyabiashara wa nje?

Supplementary Question 2

MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na nataka kujua tu, Serikali inipe majibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuzuia branding za Tanzanite externally, nayo yana sovereign ownership ya Tanzania na kuthibiti mapato ya Serikali; kulikuwa na Mkataba ambao ulisainiwa Afrika Kusini mwaka 2003 unaitwa Kimberley Process. Certification ya madini haya ilikuwa pamoja na Diamonds, kipindi kile kulikuwa na conflict diamonds, lakini waka-incorporate na madini ambayo yana thamani kama Tanzanite.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua, je, Tanzania tumo katika mkakati huo wa certification ya Tanzanite ili kudhibiti sovereign ya mali hii ibaki nchini na itambulike kuwa ni mali ya Tanzania tu? (Makofi)

Name

Prof. Sospeter Mwijarubi Muhongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Vijijini

Answer

WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Kimberley Code yenyewe ilikuwa controversial. Kuna wengine waliikubali, wengine wameikataa, ikaanzishwa nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jibu la kifupi ni ndiyo tunataka Tanzanite. Hata Ofisi yetu ya London, wale wafanyakazi wa kwetu kule waliokuwa wanasimamia uuzaji wa diamonds, wakiwa wana Ofisi London, tuliifunga, tunataka haya madini yauzwe nchini hapa. Jibu ni ndiyo!