Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 8 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 100 2016-09-16

Name

Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA N. MAKILAGI aliuliza:-
Sheria ya Ndoa imekuwa kandamizi kwa wanawake na watoto:-
Je, ni lini sheria hii italetwa Bungeni ili ifanyiwe marekebisho?

Name

Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Answer

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu:-Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Nassoro Makilagi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 ni matokeo ya mjadala mpana na shirikishi kupitia Waraka wa Serikali namba moja wa mwaka 1969. Lengo la mjadala huo lilikuwa kupata muafaka kuhusu maudhui ya sheria hiyo ambayo yaligusa imani, mila na desturi za Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya miaka zaidi ya 20 kupita tangu sheria hiyo ya ndoa itungwe, Serikali kupitia Tume ya Kurekebisha Sheria iliifanyia mapitio ya sheria hiyo na kubaini maeneo kadhaa yenye udhaifu na hivyo kuhitaji kufanyiwa marekebisho. Kutokana na maoni hayo ya Tume, Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria iliandaa mwaka 2008 Waraka wa Baraza la Mawaziri uliokuwa na mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971.
Kwa kuzingatia chimbuko la sheria hiyo, Baraza liliiagiza Wizara kuandaa Waraka Maalum wa Serikali (White Paper) ili kupata mjadala mpana na shirikishi kama ilivyokuwa awali. Mapema mwaka 2010 Wizara ilikamilisha maandalizi ya waraka huo ambao pamoja na kubainisha hoja ambazo wananchi wangetakiwa kuzitolea maoni uliainisha utaratibu wa kukusanya maoni ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Desemba, 2010 kabla waraka huo haujajadiliwa na kuridhiwa na Baraza la Mawaziri mchakato wa mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukaanza na kulilazimu Baraza kusitisha kwa muda mchakato wa marekebisho ya ndoa. Serikali ilikuwa na matarajio kuwa wakati Tume ya Mabadiliko ya Katiba inakusanya maoni ya wananchi kuhusu mabadiliko ya Katiba, wananchi wangetoa maoni kuhusu Sheria ya Ndoa, Mirathi na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kukamilisha kazi yake, ilibainika kwamba wananchi wengi hawakujielekeza kwenye maudhui ya Sheria ya Ndoa, hivyo Wizara ya Katiba na Sheria ikaamua kuendeleza juhudi za awali kwa kukamilisha taratibu za kupata maoni ya wananchi kwa utaratibu wa White Paper, zoezi hili litakamilika ndani ya muda si mrefu.