Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 19 Sitting 22 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 285 2025-05-12

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Je, lini Serikali itaweka uzio katika Hifadhi za Taifa ili kunusuru maisha ya wananchi na mali zao dhidi ya wanyamapori?

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa uhifadhi imejenga uzio wa umeme wenye urefu wa kilometa 33 kwa gharama ya dola za Kimarekani 330,000 katika mpaka wa Pori la Akiba la Ikorongo na Vijiji sita vinavyopakana na Pori hilo ambavyo ni Mbilikili, Bonchugu, Rwamchanga, Kazi, Miseke na Park Nyigoti katika Wilaya ya Serengeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile uzio wenye urefu wa kilometa 12 wenye thamani ya dola za Kimarekani 88,971.24 katika ushoroba wa Mwinihana – Magombera iliyopo Udzungwa na uzio wenye urefu wa kilometa 16 wenye thamani ya dola za Marekani 371,696 kwenye mipaka ya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na Vijiji vya Mang'ola juu, Oldeani, Mtaa wa Kambi ya Nyoka na Mtaa wa Tloma Wilayani Karatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, licha ya kujitokeza kwa uhitaji wa uwepo wa uzio katika maeneo yote ya Hifadhi nchini, tafiti za kisayansi zinaelekeza kutofanya hivyo kwa kuwa kutasababisha kuvurugika kwa mwingiliano uliopo wa wanyamapori kwenye mifumo yao ya kiikolojia hali itakayoathiri mienendo, tabia na athari kwenye mtiririko wa vinasaba vya wanyamapori na hivyo kuathiri uzalianaji na ukuaji wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muktadha huo, Serikali inaendelea kufanya tafiti na tathmini ya kina ili kuona uwezekano wa kuweka uzio kwa baadhi ya maeneo ya hifadhi hapa nchini ambayo yameathiriwa sana na wanyamapori wakali na waharibifu ikiwemo maeneo ya Bagamoyo, Mikumi, Kagera, Mkomazi na eneo la kutokea Pori la Akiba la Ikorongo kuelekea Tabora B na kutokea Pori la Akiba la Grumeti kuelekea Ndabaka.