Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 19 Sitting 23 Union Affairs Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano 295 2025-05-13

Name

Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Primary Question

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: -

Je, ni hatua gani imefikiwa katika kutekeleza taarifa ya wataalamu kuhusu Ziwa Tlawi?

Name

Khamis Hamza Khamis

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Uzini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilifanya tathmini ya kina ya hali ya mazingira ya Ziwa Tlawi na kuandaa taarifa iliyobainisha changamoto mbalimbali ambazo zinatishia uhai na uwepo wa ziwa pamoja na mifumo ya ekolojia yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hizo ni pamoja na ziwa kujaa taka kwa maana ya tope, kupungua kwa maji yanayoingia ziwani kunakotokana na uchepushwaji wa maji yote ya Mto Endayaya ambayo yanatumika kwa shughuli za majumbani na uwepo wa magugu maji ya aina mbalimbali ndani na kandokando ya ziwa, hivyo kupunguza eneo la shughuli za uvuvi pamoja na bayoanuai iliyokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na changamoto hizo, Serikali itaendelea kutenga fedha pamoja na kutafuta fedha kupitia mifuko ya hifadhi na usimamizi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ikiwemo Mfuko wa Dunia wa Hifadhi ya Mazingira (GEF) na Mfuko wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (GCF) ili kunusuru ziwa hilo na mifumo ya ikolojia yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua athari ambazo zinaweza kusababishwa na uharibifu wa Ziwa Tlawi na maziwa mengine hapa nchini, kupitia Bunge lako Tukufu, naomba kuziagiza Halmashauri zote nchini kuendelea kusimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Sura 191 Kifungu Na. 51 (4), kinachozuia uendeshaji wa shughuli za kudumu za binadamu au zenye madhara kwa mazingira ndani ya mita 60 kutoka kwenye kingo za Ziwa hilo pamoja na mito na vijito vinavyoelekeza maji katika Maziwa. Nakushukuru. (Makofi)